Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Hapa na Pale

Hapa na Pale

Mashirika ya UM ya UNICEF, WHO na washiriki wanaohudumia misaada ya kiutu yamejumuika nchini Zimbabwe kukabili maradhi ya kipindupindu yalioripotiwa kuzuka katika vitongoji vya mji mkuu wa Harare, ambapo inaripotiwa watu 11 walifariki na 80 wengine waliambukizwa na maradhi hayo. UNICEF ikishirikiana kwa ukaribu zaidi na wenye madaraka wenyeji, pamoja na mashirika yasio ya kiserikali na WHO, imenzisha vituo viwili vya matibabu kuwasaidia wagonjwa wa kipindupindu. Zahanati hizo zinaendeshwa na lile shirika la madaktari wa kimataifa lijulikanalo kama Médecins Sans Frontières.

Shirika la UM juu ya Miradi ya Kupunguza Maafa (ISDR) limeripoti kwamba mafuriko na dhoruba haribifu za karibuni zimekithirisha hali ya umaskini na ufukara katika maeneo mengi ya dunia. Salvano Briceno, Mkurugenzi wa ISDR alisema kwenye taarifa yake kwamba athari mbaya za matufani na vimbunga vya mara kwa mara, vilivyopiga karibuni katika maeneo ya Karabian na Marekani, ni matukio yenye kuonyesha dhahiri kuwepo fungamano kati ya viwango vya maendeleo katika nchi na vifo vya umma vinavyosababishwa na majanga ya kimaumbile.