Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mradi wa IFAD India waepusha uuaji wa watoto wa kike tumboni 

Mtoto wa kike akipokea chanjo dhidi ya polio kijiji cha Maliwada nchini India.
©UNICEF/Ashutosh Sharma
Mtoto wa kike akipokea chanjo dhidi ya polio kijiji cha Maliwada nchini India.

Mradi wa IFAD India waepusha uuaji wa watoto wa kike tumboni 

Haki za binadamu

Katika kuangazia harakati za kukabili ukatili dhidi ya wanawake, tunakwenda nchini India ambako harakati za mfuko wa maendeleo wa Umoja wa Mataifa, IFAD, umesaidia wakazi wa eneo la Maharashtra kuondokana na tabia ykutaka wajawazito kutoa mimba za watoto wa kike.

Nchini India, wanawake wa jamii ya Maharashra wakigonga kifaa maalum kuashiria tukio maalum la sherehe. Nalo si lingine bali ni uzao wa mtoto, lakini leo tukio hili ni la ajabu zaidi kwa kuwa sherehe ni ya kukaribisha kuzaliwa mtoto wa kike. Rupaki Pandurand Pawar ni mama mzazi. "Naitwa Rupali Pandurand Pawar. Naishi Velgaon, Karjat na nina umri wa miaka 30. Ujauzito wangu wa pili nimejingua mtoto wa kike. Nilifurahi sana, halikadhalika familia yangu. Kijijini kwetu, serikali ya kijini inafurahia uzao wa mtoto wa kike.” 

Awali sherehe kama hizi zilikuwa ni za uzao wa mtoto wa kiume na si wa kike. Tukio la leo limeandaliwa na mradi wa Tejaswini unaofadhiliwa na IFAD na serikali ya India. Mradi umejengea uwezo zaidi ya wanawake milioni moja kwa kuwajengea uwezo kifedha na kitamaduni. 

Licha ya sheria za kupiga marufuku uchunguzi wa ujauzito ili kuepusha utoaji mimba za watoto wa kike, bado sehemu nyingi nchini India kuwa na mtoto wa kike inaonekana ni jambo la kukatisha tamaa. 

Sasa mradi unataka kuhamasisha jamii kuona watoto wa kike sawa na wa kiume kama asemavyo Shraddha Joshi, Mkurugenzi kutoka IFAD.  “Sherehe kama za watoto wa kike ni muhimu sana kwetu. Zinatusaidia kwa njia nyingi. Mosi kuzuia uchaguzi wa jinsia, unaongeza kiwango cha uwiano wa jinsia. Mtazamo wa jamii nzima unabadilika. Zamani mtoto wa kike alikuwa mzigo sasa anafurahiwa.” 

IFAD inasema juhudi za pamoja kupitia mradi kama huu umeleta mafanikio makubwa na kuongeza idadi ya watoto wa kike wanaozaliwa. 

Kadri Rupali anavyopokea zawadi kutoka rafiki zake, anapata matumaini kuwa hata binti yake atakuwa anapata heshima sawa kama mtoto wake wa kiume.