Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ndoto si ndoto tu wakati mwingine hutimia:Mkimbizi Sidra

Mitaa ya mji wa Istanbul
Simone D. McCourtie / World Bank
Mitaa ya mji wa Istanbul

Ndoto si ndoto tu wakati mwingine hutimia:Mkimbizi Sidra

Wahamiaji na Wakimbizi

Hakuna faraja kubwa unayoweza kuipata kama pale ndoto zako zinapotimia, na hii ndio hali anayoihisi Sidra Taleb mkimbizi kutoka Syria aliyetamani sana kusomea udaktari wa meno, na kwa ukarimu wa serikali ya Uturuki sasa anatimiza ndoto hiyo. 

Istanbul nchini Uturuki mji wenye mandhari ya kuvutia sasa ni maskani mapya ya mkimbizi Sidra Taleb aliyefungasha virago na kukimbia Aleppo Syria mwaka 2013 kwenda kusaka usalama Uturuki , akiota kusomea udaktari wa meno siku moja.

Hivi sasa ndoto yake imetimia, asante kwa dhamira na jitihada zake lakini pia msaada mkubwa unaotolewa na serikali ya Uturuki kwa wakimbizi kupata elimu ya juu,“mimi ndiye msichana mkubwa katika familia, pia ndiye msichana wa kwanza katika familia kufanya shahada ya udaktari”

Sidra aliyepata ufadhili wa chuo kikuu cha Istanbul anasema wengi husita hata kwenda kwa kadtari wa meno lakini si yeye,“sihajwahi kuwaogopa madaktari wa meno, badala yake nawapenda na napenda udaktari wa meno. Hakuna cha kuogopesha kuhusu wao”

Sidra ni miongoni mwa takriban wanafunzi 33,000 wakimbizi wa Syria ambao kupitia msaada hivi sasa wanasoma katika vyuo vikuu nchini Uturuki na anasema wema na fadhila aliyotendewa atapenda kuilipa siku moja, “watu wenye mafanikio wanaweza kusaidia nchi wanayoishi. Uturuki imenisaidia sana na itakuwa faraja kwangu siku moja kulipa fadhila kwa watu wake na kuwa raia mchangiaji katika jamii.”

Uturuki inahifadhi wakimbizi wa Syria waliosajiliwa milioni 3.68 na kuifanya kuwa ndio nchi inayohifadhi wakimbizi wengi zaidi duniani.