Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Dunia lazima ichukue hatua kushughulikia athari za utumwa:UN

Maonyesho katika siku ya kuwakumbuka  wahanga wa biashara ya utumwa na ile ya baharí ya Atlantic kwenye makao makuu ya Umoja wa Mataifa, New York, Machi 2019
Picha na UN/ Loey Felipe
Maonyesho katika siku ya kuwakumbuka wahanga wa biashara ya utumwa na ile ya baharí ya Atlantic kwenye makao makuu ya Umoja wa Mataifa, New York, Machi 2019

Dunia lazima ichukue hatua kushughulikia athari za utumwa:UN

Masuala ya UM

Athari za utumwa na biashara ya utumwa bado zinaendelea kuonekana duniani kote hivi leo na dunia ni lazima ichukue hatua zaidi kushughulikia athari hizo. Hayo yameelezwa leo na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika hafla maalum ya siku ya kimataifa ya kuwakumbuka wahanga wa biashara ya utumwa na ile ya baharí ya Atlantic kwenye Baraza Kuu la Umoja wa huo mjini New York Marekani.

Antonio Guterres amesema utumwa ilikuwa moja ya ukatili wa kupindukia katika historia ya mwanadamu nahasa kwa watu wenye asili ya Afrika walioteseka, kupambana na hata kupoteza maisha yao wakijaribu kupigania uhuru wao kutoka kwa watesi wao. Ameongeza kuwa

(SAUTI YA ANTONIO GUTERRES)

“Watu kutoka Afrika waliofanywa watumwa, waliumizwa vibaya na mara nyingi kuuawa na taasisi ambayo haikupaswa kuwepo , lakini walikuwa zaidi ya waathirika , watumwa hao walipambana na mfumo ambao walijua haukustahili walipinga kwa nguvu zote na mara nyingi walijitolea maisha yao kwa ajili ya uhuru na utu. Hivyo tunakumbuka sio tu watu kushikiliwa bila hiyari yao bali pia ari iliyowafanya wanyanyasaji kuasi.”

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres
UN
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres

Kwa zaidi ya miaka 400 zaidi ya watu milioni 15 , wanaumme, wanawake na watoto walikuwa waathirika wa biashara hiyo haramu ya utumwa na baharí ya Atlantic. Kumbukumbu ya tarehe ya leo amesema Guterres pia ni fursa ya kuelimisha kuhusu hatari ya ubaguzi wa rango na chuki zinazomea mizizi katika karne hii na kusistiza kwamba

(SAUTI YA ANTONIO GUTERRES)

“Tunapoadhimisha siku ya kimataifa ya kumbukumbu tuamue kuubeba ujumbe wao hadi mbali zaidi, kupambana na ubaguzi wa rango, kukabili chuki dhidi ya wageni kushughulikia ubaguzi, kumaliza hali ya kutenga watu kijamii na kisiasa na kudumisha utu kwa wote. Kwa pamoja tusimame kidete kupinga aina zote mpya za utumwa kwa kuelimisha kuhusu hatari za ubaguzi wa rango katika enzi zetu na kuhakikisha hali na fursa kwa watu wote wenye asili ya Afrika hii leo.”

Naye Rais wa Baraza Kuu Maria Ferndana Espinosa akiunga mkono hayo katika hafla hiyo amesema “Wakati dunia ikiingia katika mwaka wa nne wa muongo wa watu wa asili ya Afrika tunahitaji kuongeza juhudi kushughulikia athari za historia yetu kwa watu na taasisi wakati huu.”