Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Tuzipe nafasi zaidi sauti za wanawake wa jamii za asili kwani wana mchango mkubwa duniani - Guterres 

Mkutano wa Kwanza wa Kitaifa wa Mashauriano ya Watu wa Jamii ya asili huko San José, Costa Rika, Mei 2017
OHCHR Costa Rica/Charlie Osorio
Mkutano wa Kwanza wa Kitaifa wa Mashauriano ya Watu wa Jamii ya asili huko San José, Costa Rika, Mei 2017

Tuzipe nafasi zaidi sauti za wanawake wa jamii za asili kwani wana mchango mkubwa duniani - Guterres 

Wanawake

Ikiwa leo Agosti 9 ni siku ya Kimataifa ya watu wa jamii ya asili dunani, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres kupitia ujumbe wake mahususi kwa siku hii, ametoa wito kwa ulimwengu kuzidisha zaidi sauti za wanawake wa jami ya asili kwani wana mchango mkubwa kwa ulimwengu.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres kupitia video ya ujumbe wake anaanza kwa kueleza kinachoangaziwa katika Siku ya Kimataifa ya Watu wa asili Duniani ya mwaka huu, kwani kuhusu jukumu la wanawake wa jamii za asili katika kuhifadhi na kupitisha maarifa ya jadi kutoka kizazi hadi kizazi. 

“Wanawake wa jamii za asili ni watunzaji wa maarifa ya mifumo ya chakula na dawa asilia. Ni mabingwa wa lugha na tamaduni za asili. Wanalinda mazingira na haki za binadamu za watu wa asili.” Anaeleza Guterres.  

Bwana Guterres anatoa ushauri kwamba ili kujenga mustakabali ulio sawa na endelevu ambao haumwachi mtu nyuma, lazima dunia izipe nafasi zaidi sauti za wanawake wa jamii za asili na kwamba maarifa asilia ya kitamaduni yanaweza kuleta ufumbuzi kwa changamoto zetu nyingi. 

Akitoa mfano wa hivi karibuni wa namna alivyoshuhudia haya anayoyasema, Katibu Mkuu Guterres anakumbushia alipokuwa ziarani hivi karibuni nchini Suriname, kwamba alijifunza kwa kuona kabisa jinsi watu wa jami za asili wanavyolinda msitu wao wa mvua na bainuai yake tajiri. 

Kwa msingi wa hayo yote, Katibu Mkuu anatoa wito kwamba katika Siku hii ya Kimataifa, Nchi Wanachama wa Umoja wa Mataifa watekeleza Azimio la Umoja wa Mataifa kuhusu Haki za Watu wa jamii za asili na kuendeleza maarifa asilia kwa manufaa ya wote.