Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Cheti cha kuzaliwa alichopata mwanangu kitatukomboa sote: Bernalita wa jamii ya Sama Bajau

Nchini Indonesia watu wengi hutegemea bioanuwai ya misitu ili kujipatia riziki.
CIFOR/Ulet Ifansasti
Nchini Indonesia watu wengi hutegemea bioanuwai ya misitu ili kujipatia riziki.

Cheti cha kuzaliwa alichopata mwanangu kitatukomboa sote: Bernalita wa jamii ya Sama Bajau

Haki za binadamu

Cheti cha kuzaliwa ni moja ya nyaraka muhimu kwa utambulisho wa mtu, lakini pia kigezo cha kusaidia kupata huduma za msingi kama za afya, elimu na hata hifadhi ya jamii.

Kwa mujibu wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR mambo ni tofauti sana kwa jamii ya wavuvi ya Sama Bajau inayoishi kwenye mwambao wa Ufilipino, Malaysia na Indonesia ambao kwa miaka mingi wamekosa huduma kwa kutokuwa na vyetu vya kuzaliwa. Sasa  shirika hilo limeanzisha kampeni kubadili historia hiyo.

Katika Kijiji cha Kasanyangany pwani ya Ufilipino inaishi jamii ya Sama Bajau. Asilimia kubwa ya watu wa jamii hii ni maamumma hawajui kusoma wala kuandika kisa, hakuweza kuingia shule kwa kukosa vyeti vya kuzaliwa. 

Mfumo wao wa maisha unawakosesha huduma za msingi kama kupata elimu, afya na msaada wa kijamii sababu ya kutoelewa umuhimu wa kuwa na cheti cha kuzaliwa. 

Sasa UNHCR kupitia wafanyakazi wa kujitolea wa jamii imelivalia njuga suala hili kwa kampeni kubwa ya kuhakikisha mtazamo wa jamii unabadilika.

Almalyn Akmad ni mmoja wa wafanyakazi hao na anapita nyumba kwa nyumba kusajili wakazi ili wapate vyeti 
“Kama mfanyakazi wa kujitolea ninawasaidia kwa sababu wengi wao hawajui kusoma wala kuandika, na wengine hata wanaogopa kuzungumza na wafanyakazi wa ofisi ya usajili, hivyo ninawasaidia kama mkalimani.” 

Mbali ya kuwasajili pia wanaelimisha umuhimu wa kuwa na vyeti vya kuzaliwa na baada ya kuelimika Bernalita mkazi wa jamii hii anasema “Cheti cha kuzaliwa ni muhimu kwa sababu kitatusaidia. Waalimu shuleni wanataka tuwape nakala ya cheti ili mtoto asome. Cheti kitamsaidia mwanangu Bermaisa kupata elimu.” 

Bernalita anasema ni ndoto yake ni kwa mwanaye kupata elimu ili asiwe mbumbumbu kama yeye aweze kujua kusona na kuandika. Na baada ya kupokea vyeti vyao kwa furaha kubwa bintiye Bermaisa anasema “Ninataka kumsaidia mama yangu na kusaidia watu wengine. Na pia nataka kuwa mwalimu ili niwasaidie watoto wengine wa jamii yangu.” 

Kwa UNHCR anasema Almalyn haya ni mafanikio kwani sasa jamii hii iliyobaki nyuma kwa muda mrefu inaanza kuona nuru gizani sio tu kwa kupata elimu lakini pia itaweza kupata ajira na kuwa na maisha bora na kubwa zaidi sasa inaelewa umuhimu wa vyeti vya kuzaliwa.