Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ndege ya Umoja wa Mataifa yapata ajali nchini Ethiopia

Wafanyakazi wa misaada wakiwasili Mekelle katika jimbo la Tigray nchini Ethiopia, ikiwa ni ndege ya kwanza  ya watoa huduma wa misaada kuwasili eneo hilo. ( Picha kutoka Maktaba)
© WFP/Photolibrary
Wafanyakazi wa misaada wakiwasili Mekelle katika jimbo la Tigray nchini Ethiopia, ikiwa ni ndege ya kwanza ya watoa huduma wa misaada kuwasili eneo hilo. ( Picha kutoka Maktaba)

Ndege ya Umoja wa Mataifa yapata ajali nchini Ethiopia

Msaada wa Kibinadamu

Ndege ya ofisi ya Umoja wa Mataifa la utoaji wa huduma za kibinadamu, (UNHAS) inayosimamiwa na shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula duniani -WFP imepata ajali  jana tarehe 27 mwezi huu wa Julai huko nchini Ethiopia wakati ikisafirisha watoa huduma kutoka Jigjiga kwenda Dire Dawa.

Taarifa iliyotolewa na WFP kutoka Roma nchini Italia imesema ndege hiyo ambayo ilikuwa katika safari yake chini ya  mshirika mwenza wa anga -Abyssinia Air ililazimika kutua kwa dharura kwa ajali ikiwa na watu wanne, wawili wakiwa ni watoa huduma wa shirika la madaktari wasio na mipaka (MSF) na wawili ni waendeshaji wa ndege hiyo. 

“Watu wote wanne hawajapata majeraha yoyote kutokana na ajali hiyo, na wamepelekwa katika hospitali Dire Dawa kwa ajili ya uchunguzi zaidi.” Imesema taarifa hiyo.

Bado chanzo cha ajali hiyo hakijafahamika na Abbyssinia Air, WFP na mamlaka ya anga ya ndani katika eneo hilo wanafanya uchunguzi.