Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kwa waliopitia GBV msaada wa kibinadamu pekee hautoshi wanahitaji pia wa kisaikolojia:Razia

Wanawake na watoto wasubiri msaada wa kibinadamu Cox's Bazar, Bangladesh, ambapo milioni moja ya wakimbizi wa Rohingya wamehifadhiwa.
Olivia Headon/IOM
Wanawake na watoto wasubiri msaada wa kibinadamu Cox's Bazar, Bangladesh, ambapo milioni moja ya wakimbizi wa Rohingya wamehifadhiwa.

Kwa waliopitia GBV msaada wa kibinadamu pekee hautoshi wanahitaji pia wa kisaikolojia:Razia

Haki za binadamu

Kutana na mwanamke mwanasheria na mwanaharakati wa haki za wanawake Razia Sultana ambaye ameanzisha mahala salama kwenye kambi ya Cox’s Bazaar nchini Bangladesh kwa ajili ya kuwapa msaada wa kisaikolojia wanawake wakimbizi wa Rohingya kutoka Myanmar waliopitia ukatilia wa kijinsia au GBV.

Katika kambi kubwa kabisa ya wakimbizi wa Rohingya ya Cox’s Bazar Razia akielekea ofisini kwake kwenye kituo cha Shanti Khana jina likimaanisha "kituo cha amani" tayari kwenda kutoa ushauri nasaha ambao ni muhimu sana kwa mamia ya wanawake na wasichana wakimbizi wa Rohingya waliopitia ukatili wa hali ya juu wa kijinsia ambao umewafanya wengi kuchanganyikiwa na kuishi na majinamizi.  

Razia anasema kilichomsukuma hata kufungua kituo hiki ni hadithi za kutisha na kusikitisha alizozisikia kutoka kwa wanawake na wasicha hao,“Niliwahoji wanawake zaidi ya 300 waathirika wa ubakaji na nikaona shikizo linalowakabili, mwanamke mmoja aliniomba msaada sababu alitaka kujiua nilishtuka sana, na msichana mwingine mmoja niliyeongea naye pia alijaribu kujiua mara mbili kwa sababu hakutaka kuzungumzia aibu ambayo ni ya familia nzima, alidhani anachukiwa kwani amebakwa na hatakiwi kwenye familia na jamii yake, nikampa ushauri nasaha na kumwambia la hasha ,hakuna anayekuchukia na hili si kosa lako” 

Razia anasema jamii ya Rohingya ni yenye misimamo ya kizamani na ukatili wa kijinsia au GBV unachukuliwa kama sehemu ya maisha ya jamii hiyo yenye utamaduni wa kiislam hivyo anaona ni muhimu sana kuchukua hatua kuwalinda wanawake hawa hasa wasio na elimu ambao mara nyingi huachwa nyuma katika ajira na hata kipato ingawa wanapatiwa misaada na mashirika ya kibinadamu na mashirika ya misaada , lakini misaada hiyo haitoshi kwa sababu ya athari za kisaikolojia waliozipata."kile kinachotakiwa hasa katika program za GBV hawakitoi , kwa sababu program za GBV zinahitaji ushauri nasaha, jinsi gani tunaweza kuuzuia ukatili huu, tunahitaji ujuzi kuuzuia lakini hawafanyi hiyo, wanachofanya ni kama kusema tu usimuumize mkeo, usipige watoto wako, usimpige mkeo, usiowe wake wengi hii ni kama hotuba tu iliyoandikwa kitabuni.” 

Kwa sababu hiyo Raza anafanyakazi kwa karibu na wanau mbalimbali yakiwemo mashirika ya Umoja wa Mataifa kuhakikisha kwamba wanawake hawa wakimbizi wa Rohingya mbali ya misaada ya mahitaji muhimu ya kibinadamu wanapatiwa msaada wa kisaikolojia ambao utawasaidia kutimiza usemi yaliyopita si ndwele tugange yajayo .