Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UNICEF yakaribisha kuachiwa huru kwa watoto 10 kutoka katika vikosi vya kujihami Sudan Kusini

Watoto Sudan Kusini
UNMISS/Ilya Medvedev
Watoto Sudan Kusini

UNICEF yakaribisha kuachiwa huru kwa watoto 10 kutoka katika vikosi vya kujihami Sudan Kusini

Amani na Usalama

Watoto kumi wenye umri kati ya miaka 15 na 17, wameachiwa huru kutoka katika makundi yenye silaha nchini Sudan Kusini, shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF, imeeleza leo katika mji mkuu wa nchini hiyo, Juba.

Wavulana tisa na msichana mmoja wametambuliwa katika moja ya vituo vya mafunzo kwa ajili ya vikosi vilivyounganishwa, katika mji mkuu Juba. Kamisheni ya kitaifa ya upokonyaji silaha na kuwarejesha watu katika maisha ya kawaida ya kijamii nchini Sudan Kusini NDDRC, Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini humo, UNMISS na UNICEF, wamewezesha kuachiliwa kwa watoto hao kwa kusaidiwa na vikosi vya ulinzi wa raia wa Sudan Kusini, SSPDF.

 Wakati muda wa kuhitimu unapokaribia katika vituo vya mafunzo, ilikuwa muhimu kwa NDDRC, UNMISS na UNICEF kuwaondoa watoto katika maene hayo yaliyotengwa.

 Watoto wanahifadhiwa kwa muda katika vituo vya huduma ambako wanakuwa wakihudumiwa katika kipindi ambacho familia zao zinatafutwa. Watoto pia watapokea msaada utakaowawezesha kupata mahitaji ya msingi kama vile nguo mpya, vitatu, sabuni na mahitaji mengine. Pia watapatiwa msaada wa kisaikolojia, taarifa imefafanua.

Mwakilishi wa UNICEF nchini Sudan Kusini Mohamed Ag Ayoya amesema, “jeshi lililounganishwa lina msimamo wa wazi na wa pamoja dhidi ya matumizi ya watoto katika vikosi vyenye silaha na makundi ya kujihami.Ninayo furaha kuona kuwa vikosi vyenye silaha vinaendelea kufanya kazi na NDDRC, UNMISS na UNICEF kuwaachia watoto kutoka katika majeshi na kuwaruhusu kurejea nyumbani katika familia zao ambako ndiko wanastahili kuwa.”

 UNICEF inasema baadhi ya kambi za kijeshi na kambi za mafunzo nchini Sudan Kusini zina msongamano mkubwa wa wat una kukosa miundombinu ya kujisafi na hivyo katika muktadha wa mlipuko wa ugonjwa wa COVID-19, kuwaruhusu watoto kurejea katika familia zao itakuwa salama kwa watoto hao.