Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Nyuki wako hatarini, uhakika wa chakula nao mashakani- FAO

Nyuki akichavua ua kwenye mti wa mkaratusi katika kituo cha utafiti wa misitu cha Chesa mjini Bulawayo nchini Zimbabwe.
FAO/Zinyange Auntony
Nyuki akichavua ua kwenye mti wa mkaratusi katika kituo cha utafiti wa misitu cha Chesa mjini Bulawayo nchini Zimbabwe.

Nyuki wako hatarini, uhakika wa chakula nao mashakani- FAO

Malengo ya Maendeleo Endelevu

Leo ni siku ya nyuki duniani ambapo shirika la chakula na kilimo la Umoja wa Mataifa, FAO linatumia siku hii kuangazia athari za janga la ugonjwa wa virusi vya Corona au COVID-19 katika uzalishaji na biashara ya zao hilo.
 

FAO kupitia wavuti wake inasema inatambua kuwa “janga la sasa la COVID-19 limekuwa na athari za dhahiri katika sekta ya ufugaji nyuki, likiathiri uzalishaji, masoko na matokeo yake ni kuathiriwa kwa maisha ya wafugaji wa nyuki.”

Ni kwa mantiki hiyo FAO inasema kuwa itatumia tukio la leo litakalofanyika kwa njia ya video, kuangazia dhima ya ufugaji nyuki katika kusaidia jamii za vijijini na kuboaresha upatikanaji wa chakula na lishe hasa wakati huu wa sasa wa janga la Corona.

FAO kupitia maudhui yake ya jishirikishe, itamulika umuhimu wa elimu ya asili inayohusiana na ufugaji wa nyuki na matumizi ya bidhaa na huduma zitokanazo na nyuki na umuhimu wake katika kufanikisha malengo ya maendeleo endelevu, SDGs.

Mathalani, uzalishaji wa nyuki na mifano bora inayotumiwa na wafugaji wa nyuki katika kusaidia kujipatia kipato na kuhakikisha wanakuwa na bidhaa zenye ubora.

Je wafahamu wadudu na ndege wachavushaji ?

Siku hii pia itatumia kuhamasisha na kuelimisha umma kuhusu umuhimu wa wadudu na ndege wachavushaji na tishio wanalokumbana nalo katika mchango wao wa kufanikisha malengo ya maendeleo endelevu, SDGs.

FAO inasema kuwa nyuki, ambao ni wachavushaji wakuu miongoni mwa wengine kama vile popo na ndege, hivi sasa wako hatarini kutokana na shughuli za binadamu.

“Uhai wa wadudu wachavushaji unategemea bayonuia ya dunia.Takribani asilimia 90 ya mimea yenye maua hutegemea kwa kiasi kikubwa uchavushaji sambamba na zaidi ya asilimia 75 ya mazao ya chakula n asilimia 35 ya ardhi ya kilimo,” imesema FAO.