Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mlinda amani wa UN auawa Mali, 4 wajeruhiwa, Guterres azungumza

Walinda amani kutoka Chad wakipiga doria katika mitaa ya Kidal nchini Mali.(maktaba Desemba 2016)
MINUSMA/Sylvain Liecht
Walinda amani kutoka Chad wakipiga doria katika mitaa ya Kidal nchini Mali.(maktaba Desemba 2016)

Mlinda amani wa UN auawa Mali, 4 wajeruhiwa, Guterres azungumza

Amani na Usalama

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amelaani vikali mashambulio mawili dhidi ya ujumbe wa umoja huo wa kuweka utulivu nchini Mali, MINUSMA ambayo yamesababisha kifocha mlinda amani mmoja huku wengine wanne wakijeruhiwa.

Habari zinasema mlinda amani huyo kutoka Chad aliuawa na wenzake watatu walijeruhiwa sana wakati msafara wao ulipokanyaga kilipuzi kwenye eneo la Aguelhok, lililoko huko Kidal kaskazini mwa Mali.

Mapema katika tukio lingine, watu wasiojulikana walishambulia kambi ya muda ya MINUSMA huko Bandiagara jimboni Mopti, katikati mwa Mali na kusababisha mlinda amani mmoja kutoka Togo kujeruhiwa.

Kupitia taarifa ya msemaji wake iliyotolewa leo jijini New York, Marekani, Katibu Mkuu Guterres amesihi mamlaka za Mali pamoja na vikundi vilivyojihami ambavyo vilitia saini makubaliano ya amani yam waka 2015, wafanya juhudi zote kusaka washambuliaji ili hatua za kisheria ziweze kuchukuliwa haraka.

Makubaliano hayo ya amani yalitiwa saini na serikali ya Mali na vikundi viwili kaskazini mwa Mali vilivyojihami kwa lengo la kumaliza mzozo ulioibuka mwaka 2012.

Halikadhalika Katibu Mkuu ametuma salamu za rambirambi kwa familia ya mlinda amani aliyefariki dunia pamoja na serikali na wananchi wa Chad huku akiwatakia ahueni ya haraka majeruhi.