Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ukosefu wa usalama wachochea wimbi jipya la wakimbizi wa ndani Nigeria

Watoto kutoka katika familia zilizoparaganyika katika eneo la Maiduguri, jimboni Borno, kaskazini mashariki mwa Nigeria wakikinga maji. Mgogoro katika eneo hilo umewalazimisha mamia ya maelfu kuyahama makazi yao na kuishi kwa kutegemea misaada.
UNICEF/Gilbertson VII Photo
Watoto kutoka katika familia zilizoparaganyika katika eneo la Maiduguri, jimboni Borno, kaskazini mashariki mwa Nigeria wakikinga maji. Mgogoro katika eneo hilo umewalazimisha mamia ya maelfu kuyahama makazi yao na kuishi kwa kutegemea misaada.

Ukosefu wa usalama wachochea wimbi jipya la wakimbizi wa ndani Nigeria

Amani na Usalama

Huko Nigeria imeelezwa kuwa maeneo ya kaskazini-mashariki mwa nchi hiyo kwenye jimbo la Borno yameshuhudia idadi kubwa ya wimbi la wakimbizi wa ndani katika wiki ya mwisho ya mwaka jana.

Shirika uhamiaji la Umoja wa Mataifa, IOM limesema wimbi hilo la wakimbizi linafuatia mapigano kati ya vikundi vilivyojihami na jeshi la Nigeria kwenye jimbo hilo.

Takribani wakimbizi wa ndani 8,248 wamewasili katika miji ya Maiduguri, Baga, na Kukawa na tayari wamepatiwa  misaada ya kibinadamu ikiripotiwa kuwa wengi wao tangu wamewasili hawana makazi pamoja na huduma za msingi za kujisafi.

Mchanganuo wa taarifa ya IOM unaonyesha kuwa kambi moja huko Maiduguri imepokea kaya 1,517 au jumla ya watu 5,824 ilhali huko Baga jumla ya watu 1,779 wamepatiwa hifadhi.

Katika kambi ya Madinatu kwenye jimbo hilo la Borno wakimbizi wa  ndani 1,868 walipokelewa k utoka eneo la Baga ambako hali ukosefu wa usalama imeshamiri.

Wakimbizi hao wa ndani wengi wao wakisema kuwa kata ya Baga huko Kukawa ndio makazi yao ya awali na kilichochochea wakimbie ni mashambulizi kwenye eneo lao sambamba na ukosefu wa usalama.

Tafadhali iwapo unataka kupokea taarifa kutoka UN News Kiswahili kila wakati zinapochapishwa, tafadhali jisajili na pia unaweza kupakua apu ili kuweza kusikiliza wakati wowote popote ulipo.