Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wabobezi wakutana Italia kuamua kiwango cha kemikali kwenye vyakula

Wavuvi wakipakua samaki aina ya jodari kwenye moja ya viwanda vya kuchakata samaki huko Abidjan, Côte d’Ivoire.
FAO/Sia Kambou
Wavuvi wakipakua samaki aina ya jodari kwenye moja ya viwanda vya kuchakata samaki huko Abidjan, Côte d’Ivoire.

Wabobezi wakutana Italia kuamua kiwango cha kemikali kwenye vyakula

Afya

Wataalamu wa masuala ya viwango vya vyakula wanakutana Roma, Italia wakiangazia ni kiwango gani cha kemikali ni sahihi kwa afya ya binadamu katika chakula.

Naibu Mkurugenzi Mkuu wa shirika la chakula na kilimo duniani, FAO Maria Helena Semedo amefungua mkutano wa 41 wa kamisheni ya kimataifa inayohusika na uwekaji wa viwango vya viambato na kemikali kwenye vyakula akisema changamoto ya sasa ni  upatikanaji wa chakula cha kutosha.

Bi. Semedo amesema ni kwa mantiki wajumbe wa kamisheni hiyo wanapoangazia suala la viwango vya usalama wa chakula waende mbali zaidi kuhakikisha chakula kiko salama, kanuni za usalama zinazingatiwa na pande zote na pia kuna biashara sawia.

“Usalama wa chakula ni kichocheo kikubwa cha wazalishaji kupata masoko na pia huchagiza maendeleo ya kiuchumi na kuondokana na umaskini,” amesema Bi. Semedo.

Wakati wa kikao hicho wajumbe wa kamisheni  hiyo ambayo inatekeleza kanuni zilizoandaliwa kwa pamoja na FAO na shirika la afya duniani, WHO watapitisha viwango kadhaa.

Mathalani kiwango cha juu cha Cadmium kwenye chokoleti, kiwango cha madini ya risasi na zebaki  kwenye vyakula kama vile samaki na ukomo wa kiwango cha masalia ya dawa za kuua wadudu kwenye vyakula.