Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Tushikamane tusongeshe haki za watu wenye ulemavu wa ngozi- UN

Mtoto ambaye haoni na pia ana ulemavu wa ngozi akisoma kitabu kilichochapishwa kwa nukta nundu kwenye shule ya watoto wenye ulemavu huko Moshi mkoani Kilimanjaro.
UNICEF/Pirozzi
Mtoto ambaye haoni na pia ana ulemavu wa ngozi akisoma kitabu kilichochapishwa kwa nukta nundu kwenye shule ya watoto wenye ulemavu huko Moshi mkoani Kilimanjaro.

Tushikamane tusongeshe haki za watu wenye ulemavu wa ngozi- UN

Haki za binadamu

Ikiwa leo ni siku ya kimataifa ya kuelimisha jamii kuhusu watu wenye ulemavu wa ngozi au Albino, Umoja wa Mataifa unapigia chepuo zaidi harakati za kulinda kundi hilo ili liweze kuishi kwa amani bila woga.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres katika ujumbe wake wa siku hii ametaja hatua hizo kuwa ni pamoja na Mpango wa utekelezaji wa Afrika kuhusu Albino uliopitishwa na kamisheni ya haki za binadamu ya Afrika na bunge la Afrika.

Hata hivyo amesema hatua zaidi zapaswa kuchukuliwa duniani kote ili kuongeza uelewa wa madhila yanayokumba wanawake na wanaume wenye ulemavu huo wa ngozi ambao hupata watu bila kujali jinsia, rangi au kabila.

Jimboni Equateur nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, ulemavu wa ngozi ni jambo la kawaida na jamii hujumuika pamoja.
UN /Marie Frechon
Jimboni Equateur nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, ulemavu wa ngozi ni jambo la kawaida na jamii hujumuika pamoja.

Katibu Mkuu amesema ajenda 2030 ya maendeleo endelevu imetoa ahadi ya kutokumwacha nyuma mtu yeyote.

Kwa mantiki hiyo ametaka siku ya leo iwe fursa ya kutangaza mshikamano na watu wote duniani wenye ulemavu wa ngozi na kushirikiana kusongesha haki zao ili waweze kuishi kwa amani bila ubaguzi, wahamasike na wafurahie kikamilifu haki za binadamu.