Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Vikosi vya usalama DRC vyanyooshewa kidole

Askari wajaribu kudhibiti maandamano Goma nchini DRC kwa njia ya amani. Picha: UM/Video capture

Vikosi vya usalama DRC vyanyooshewa kidole

Amani na Usalama

Takriban watu 47 wakiwemo watoto na wanawake walipoteza maisha wakati vikosi vya usalama nchini Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo (DRC) vilipokuwa vinazima maandamano kati ya Januari Mosi 2017 na 31 Januari 2018, imesema ripoti mpya ya Umoja wa Mataifa. 

Ripoti hiyo iliyotolewa leo  katika miji ya Geneva na Kinshasa, inaorodhesha  mauaji na ukiukwaji mwingine wa haki za binadamu uliofanywa na  vikosi vya usalama katika mazingira ya kuzima maandamano.

Ripoti inasema kuna ishara kwamba vikosi vya usalama vya DRC vimejaribu kufunika  ukiukwaji huo kwa kuondoa miili ya waathirika na pia kuzuia kazi za  wachunguzi wa kitaifa na kimataifa.

Mjumbe maalum wa katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa  nchini DRC, Leila Zerrougui amesema ripoti inamulika mapengo ya kutowajibika, muendelezo wa kudidimiza demokrasia katika nchi ambayo imekuwa ikichunguzwa tangu mwanzo wa mwaka 2015, akisema

“Hii inakwenda kinyume na makubaliano ya mkataba wa  Disemba 31 mwaka 2016 na hatua zake za kujenga imani. Maandamano yanambatana na uhuru wa kujieleza na ni muhimu kuwa sauti zote zisikilizwe katika muktadha wa uchaguzi mkuu ujao.,”

Ripoti ambayo imechapishwa kwa pamoja na  ofisi ya Umoja wa Mataifa ya haki za Binadamu pamoja na ile ya kikosi cha kulinda amani cha Umoja wa mataifa nchini DRC-MONUSCO inaeleza kutoheshimu  misingi ya sheria za kitaifa na kimataifa, hasahasa ile misingi ya uhalali, mahitaji, kiasi gani cha kutumia, tahadhari na uwajibikaji ambavyo vinahusika na matumizi ya  nguvu  na vikosi vya usalama wakati wa kukabiliana na maandamano ya amani kati ya januari 2017 na januari ya mwaka 2018.