Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kizuri kwa Afrika, ni kizuri kwa ulimwengu- Ban

Kizuri kwa Afrika, ni kizuri kwa ulimwengu- Ban

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-moon, amesema kuwa utekelezaji wa ajenda 2030 kuhusu maendeleo endelevu na ajenda ya Muungano wa Afrika ya mwaka 2063, utahitaji ubia mpya wa ushirikiano wa maendeleo baina ya nchi za Afrika, Umoja wa Mataifa, AU, NEPAD, na jumuiya za kikanda.Taarifa kamili na John Kibego

(Taarifa ya Kibego)

Ban amesema hayo katika ujumbe wake wa kuadhimisha Siku ya bara Afrika, leo Mei 25, akiongeza kuwa kilicho kizuri kwa Afrika ni kizuri kwa dunia nzima.

Katibu Mkuu amesema uchumi wa Afrika unatabiriwa kukua kwa asilimia 4.4 mwaka 2016, ikilinganishwa na asilimia 3.7 mwaka 2015. Kwa mantiki hiyo, ametoa wito kwa viongozi wa Afrika watumie ufanisi huo unaotarajiwa kushughulikia tofauti za kiuchumi na kijamii zinazoendela kukua kati ya walio nacho na wasio nacho, na kuhakikisha kuwa hakuna Mwafrika anayeachwa nyuma.

Ban amesisitiza kuwa kushughulikia tofauti hizo ni muhimu katika kukabiliana na vyanzo vya mizozo, ugaidi, itikadi kali katili, na kuendeleza amani na ustawi.