Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Watoto 6000 wametumikishwa jeshini CAR, miongoni mwao ni wa kike

Watoto 6000 wametumikishwa jeshini CAR, miongoni mwao ni wa kike

Idadi ya watoto waliotumikishwa kwenye vikundi vyenye silaha huko Jamhuri ya Afrika ya Kati inaweza kufikia Elfu Sita, na hiyo ni kwa mujibu wa shirika la kuhudumia watoto la Umoja wa Mataifa, UNICEF. Grace Kaneyia na ripoti kamili.

 (Ripoti ya Grace)

 UNICEF inasema ghasia na ukosefu wa usalama nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati vimesababisha watoto waliotengana na familia zao au wenye fursa ndogo ya kupata huduma muhimu kama vile afya na elimu kuwa hatarini zaidi kutumikishwa kwenye vikundi hivyo.

Hata hivyo habari njema ni kwamba Alhamisi, UNICEF iliweza kuwakomboa watoto 23 kutoka vikundi hivyo kwenye mji mkuu Bangui na miongoni mwao ni wasichana Sita wenye umri kati ya miaka 14 na 17.

Msemaji wa UNICEF mjini Geneva, MArixie Mercado amesema watoto hao waliweza kuachiwa huru baada ya mazungumzo kati ya wawakilishi wa Umoja wa Mataifa na mamlaka za mamlaka za mpito ya kuruhusu kufikia vituo vya kijeshi ili watoto waliomo kwenye vikundi ikiwemo wafuasi wa zamani wa Seleka waachiwe huru na kukabidhiwa watetezi wa haki za mtoto.

 (Sauti ya Marixie)

“Janga la mwaka uliotangulia huko Jamhuri ya Afrika ya Kati limechochea hali ngumu ya ulinzi wa kibinadamu yenye machungu kwa watoto. Idadi ya waliotumikishwa jeshini yadaiwa imeongezeka kutokana na ongezeko la mapigano na kuibuka kwa vikosi pinzani kama vile vinavyopinga balaka. UNICEF inashirikiana na wadau wote kwenye mzozo huo kuthibitisha idadi ya watoto waliotumikishwa, na hatimaye waachiwe huru na kuungana na familia zao. Tunatiwa moyo na ushirikiano kutoka mamlaka za mpito na tunaendelea kushirikiana ili watoto waachiwe huru bila kuchelewa.”

Watoto 23 walioachiliwa huru wako kwenye kituo kinachopata usaidizi kutoka UNICEF na wanapatiwa stadi kama vile za michezo wakati wakisubiri kuungana na familia zao.