Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Visa vingine 7 vya mafua ya A H7N9 vyabainika kwa binadamu China:WHO

Visa vingine 7 vya mafua ya A H7N9 vyabainika kwa binadamu China:WHO

Tume ya kitaifa ya afya na mpango wa familia Uchina imelifahamisha shirika la afya duniani WHO kuthibitishwa kwa visa vingine saba vya maambukizi ya virusi vya mafua ya ndege, A(H7N9) kwa binadamu.

Tarehe 4 Januari taarifa ya kuugua kwa ajuza wa miaka 86 mjini Shangai zililipotiwa kwa WHO. Alianza kuumwa Desemba 26 na kulazwa hospital Desemba 30, hivi sasa hali yake imeelezwa kuwa mahtuti.

Wengine sita ni mwanamke wa miaka 34 kutoka mjini Shaoxing jimbo la Zhejiang, mwanaume wa miaka 47 kutoka jimbo la Guangdong, mkulima wa miaka 71 kutoka Yangjiang, mwanamke kutoka jimbo la Jiangsu, mwanaume wa miaka 31 kutoka Shenzhen na mwanamke wa miaka 51 kutoka mji wa Foshan ambao wote wako mahtuti hospitali.

Inasemekana wote wamekuwa karibu na kuku ingawa chanzo cha maambukizi hayo kwa mujibu wa WHO bado kinachunguzwa na hadi sasa hakuna ushahidi wa maambukizi miongoni mwa binadamu.