Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Tanzania yataka kujadiliana na UM kuhusu vikosi vya UNAMID

Tanzania yataka kujadiliana na UM kuhusu vikosi vya UNAMID

Serikali ya Tanzania imesema kuwa itaanza majadiliano ya Umoja na Mataifa ili kurekebisha kipengele kinachohusu vikosi vya ulinzi wa amani vilivyoko katika jimbo la Darfur nchini Sudan.Tanzania inataka vikosi hivyo vipewe mamlaka za kutumia nguvu ya ziada kupambana na makundi ya waasi ambayo yanavuruga ustawi wa eneohilo.(George Njogopa na taarifa zaidi)

Hatua ya Tanzania kutaka kuanzisha majadiliano na Umoja wa Mataifa inakuja kufuatia kuuwawa kwa askari wake saba walioshambuliwa na kundi la waasi wakati wakiwa kwenye msafara moja, kaskazini mwa Darfur.

Msemaji wa Jeshi la wananchi JWTZ Kanali Kapambala Mgawe amesema kuwa, kujirudia kwa matukio ya kushambuliwa kwa vikosi vya ulinzi wa amani,kunaweka ulazima wa kuangalia upya muundo wa vikosi vinavyotumwa kwenye eneo hilo.

Tanzania imetuma askari 850 ambao ni sehemu ya vikosi vya pamoja, baina ya Umoja wa Afrika na Umoja wa Mataifa UNAMID vinavyoendesha operesheni ya amani Darfur nchini Sudan.

Tayari baraza la usalama la Umoja wa Mataifa na kamishna ya Umoja wa Afrika imelaani shambulizi hilo ambalo limeacha askari wengine 17 wakiwa wamejeruhiwa.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon ameitaka serikali ya Sudan kuanzisha uchunguzi ili kuwabaini wahusika wake.