Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UNMISS yakaribisha azimio la amani Sudan Kusini

UNMISS yakaribisha azimio la amani Sudan Kusini

Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini, UNMISS, umekaribisha azimio la amani baina ya seikali ya Sudan Kusini na makundi yenye silaha nchini humo.

Katika taarifa ilotolewa siku ya Ijumaa, kundi la South Sudan Liberation Army (SSLA), na lile la South Sudan Democratic Army (SSDA) na South Sudan Defense Forces (SSDF) yalitangaza kuwa kuanzia Aprili 26 2013, vikosi vyao vitaanza kujumuika na vikosi vya serikali, Sudan Peoples Liberation Army, SPLA bila kupigana ili kuleta amani nchini mwao.

Kufuatia tangazo hilo, vikosi vya makundi hasimu vimeamrishwa kwenda kwenye sehemu zinazodhibitiwa na SPLA ili kufikia lengo hilo la amani.

UNMISS imetoa wito kwa makundi yalosalia kuiga yalofanya haya matatu, na kusema i tayari kusaidia katika hatua hii, ikiwemo kuwaondoa watoto katika makundi hayo yenye silaha na kuisaidia serikali ya Sudan Kusini kufikia amani ya kudumu.