Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Majeshi ya Sudan yadhibiti mji wa Labado:UNAMID

Majeshi ya Sudan yadhibiti mji wa Labado:UNAMID

Vikosi vya pamoja vya Umoja wa Mataifa na muungano wa Afrika vya kulinda amani Darfur UNAMID vimesema vimepokea taarifa Jumanne asubuhi kwamba majeshi ya Sudan yanayoungwa mkono na Popular Defense Forces na kundi lingine lenye silaha yamechukua udhibiti wa mji wa Labado katika jimbo la Darfur Mashariki.Vikosi hivyo vilichukua usukani kutoka kundi la Sudan Liberation Movement / Minni Minawi au (SLA/MM) baada ya mapigano makali yaliyosababisha vifo vya raia wanne na kujeruhi wengine sita.

Majeruhi hao wanapatiwa matibabu na timu ya UNAMID karibu na Labado ambako watu 8000 waliotawanywa na machafuko wanahifadhiwa tangu April 6 mwaka huu yalipozuka mapigano kati ya vikosi vya serikali na SLA/MM.

Kwa mujibu wa UNAMID hali ndani na katika viunga vya mji wa Muhajeria Mashariki mwa Darfur ingawa imetulia lakini bado kuna hofu.

Tangu April 6 raia zaidi ya 10,000 wamekuwa wakikusanyika katika eneo la UNAMID karibu na mji huo. Mkuu wa UNAMID Bwana Mohamed Ibn Chambas amezitaka pande zote kuwalinda raia na kuheshimu sheria za kimataifa na haki za binadamu.

Pia ametoa wito wa kusitishwa mapigano na kuruhusu misaada ya kibinadamu kuingizwa Mohajeria and Labado, ikiwemo katika maeneo ya timu ya UNAMID katika miji yote.