Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Shambulizi au mlipuko wa nyuklia unaweza kusababisha baa la kibinadamu: OCHA

Shambulizi au mlipuko wa nyuklia unaweza kusababisha baa la kibinadamu: OCHA

Kuna haja ya kuzingatia kwa pamoja jinsi mifumo iliyopo sasa ya huduma za kibinadamu zinavyoweza kukabiliana ipasavyo na shambulizi au mlipuko wa nyuklia, ikiwa hali hiyo ingetokea, amesema Bwana Rashid Khalikov, Mkurugenzi wa Ofisi ya Kuratibu Misaada ya Kibinadamu, OCHA, mjini Geneva.

Katika taarifa kwa waandishi wa habari wakati wa kufunguliwa kwa kongamano la kimataifa kuhusu athari za kibinadamu za zana za kinyuklia mjini Oslo, Norway, Bwana Khalikov amesema shambulizi la kinyuklia linaweza kuwa na madhara makubwa na kusababisha janga la kibinadamu.

Kongamano hilo la siku mbili linaangazia kile ambacho jamii ya kimataifa inaweza kufanya ili kujiandaa kukabiliana na athari za tukio kama hilo. Bwana Khalikov amesema kwa sasa, hakuna uwezo wa kukabiliana na athari za tukio kama hilo, na hivyo muhimu zaidi ni kuhakikisha silaha za nyuklia hazitumiki.