Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Nchi za Asia Pasifiki zaridhia mpango wa kujenga jamii inayojumuisha walemavu

Nchi za Asia Pasifiki zaridhia mpango wa kujenga jamii inayojumuisha walemavu

Mataifa 39 ya Asia-Pasifiki yameridhia kuanzisha muundo wenye lengo la kujenga jamii inayojumuisha watu wenye ulemavu kwenye ukanda huo wenye walemavu zaidi ya Milioni 650.

Makubaliano hayo yanayoitwa mkakati wa muongo mmoja wa Incheon yamefikiwa mwishoni mwa mkutano wa aina yake wa masuala ya Umoja wa mataifa kwenye ukanda huo huko Korea Kusini ambapo ulitathmini muongo mmoja uliopita wa utekelezaji wa mpango wa miaka kumi ulioanza mwaka 2003 kuhusu watu wenye ulemavu.

Tume ya Umoja wa Mataifa kuhusu masuala ya uchumi na kijamii kwa nchi za Asia na Pacific, ESCAP iliandaa mkutano huo uliohitimishwa jana ambao mwenyeji ilikuwa serikali ya Korea Kusini.

Akizungumza wakati wa kufunga mkutano huo, Naibu Katibu Mtendaji wa ESCAP Shun-Ichi Murata amesema tume yake inaunga mkono mchango wa mkakati wa Incheon kwa ajenda ya maendeleo baada ya mwaka 2015 na kushukuru washiriki kwa michango yao kuhusu watu wenye ulemavu, mchango ambao amesema utabadili maisha ya watu wenye ulemavu huko Asia-Pasifiki.

Mkakati wa Incheon wa mwaka 2013- 2022 pamoja na mambo mengine unalenga kupunguza umaskini miongoni mwa watu wenye ulemavu, kuharakisha kuridhiwa na kutekelezwa kwa mkataba wa kimataifa wa haki za watu wenye ulemavu na unajumuisha malengo na viashiria vinavyopimika miongoni mwa nchi za Asia na Pasifiki.