Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Hapa na Pale

Hapa na Pale

Ripoti ya KM iliotumiwa Baraza la Usalama juu ya hali katika Cote d’Ivoire imedhihirisha kurejea kwa utulivu na amani nchini kufuatia utiaji sahihi wa yale Mapatano ya Ouagadougou mnamo miezi 18 iliopita. Utekelezaji wa mpango wa amani nchini humo, ilisisitiza ripoti, umepiga hatua ya kutia moyo iliorahisisha usajili wa wapiga kura uliofanyika tarehe 15 Septemba.KM anatumai uchaguzi utafanyika kwa uwazi utakaoridhisha makundi husika yote katika Cote d\'Ivore.

Ofisi ya UM juu ya Misaada ya Dharura (OCHA) imetahadharisha ya kwamba hali ya chakula imeharibika sana kwenye baadhi ya majimbo Ethiopia. Kwenye ameneo hayo bei ya mahindi, mazao yenye kujumlisha chakula kikuu kwa asilimia kubwa ya raia, imepanda kwa kima kisichomudika, sawa na asilimia 275 katika baadhi ya maeneo, tukilinganisha na bei ilivyokuwa katika kipindi hicho mwaka 2007. OCHA imeripoti uhamaji wa wakazi wa vijijini wanaotafuta chakula kwenye miji umekithiri pamoja na kuongezeka kwa matatizo ya maji. Vile vile OCHA inaripoti kushuhudia utapiamlo mbaya miongoni mwa raia katika sehemu fulani za nchi.