Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Badala ya kutomwacha yeyote nyuma tunahatarisha kuyaacha malengo ya SDGs nyuma: Guterres

Mkutano wa SDG unaendelea katika ukumbi wa Baraza Kuu kwenye Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa mjini New York.
UN Photo/Cia Pak
Mkutano wa SDG unaendelea katika ukumbi wa Baraza Kuu kwenye Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa mjini New York.

Badala ya kutomwacha yeyote nyuma tunahatarisha kuyaacha malengo ya SDGs nyuma: Guterres

Malengo ya Maendeleo Endelevu

Muda wa kuchukua hatua ni sasa kuhakikisha tunayaokoa malengo ya maendeleo endelevu SDGs ambayo yanasuasua na kuwa kwenye hatari kubwa ya kutotimizwa amesema leo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres akizungumza katika ufunguzi wa jukwaa la ngazi ya juu la kisiasa kuhusu malengo ya maendeleo endelevu SDG linaofanyika kwenye Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa  jijini New York Marekani chini ya mwamvuli wa Kikao cha 78 cha Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa au UNGA78.

Katibu Mkuu amesema ahadi iliyotolewa na viongozi wa Dunia miaka 8 iliyopita kwa watu ya kuwa na Dunia yenye afya, maendeleo na fursa kwa wote inakwenda mrama na hadi sasa ni asilimia 15 pekee ya malengo 17 yaliyopitishwa ndio yako kwenye msitari unaotakiwa  menggine yanarudi nyuma na mengi yanajikongoja.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres akihutubia wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa SDG.
UN Photo/Cia Pak
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres akihutubia wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa SDG.

Kusuasua kwa malengo hayo

Viongozi wa Dunia waliafikiana na kupitisha malengo hayo 17 mwaka 2015  wakiahidi kutomwacha yeyote nyuma.

Malengo hayo yanajumuisha kutokomeza umasikini, kutokomeza njaa, kuhakikisha fursa ya upatikanaji wa maji safi na usafi lakini pamoja na kutoa elimu bora kwa wote na fursa za muda mrefu za kusoma. 

Kila lengo kuu lina vipengele vyake na jumla ya ni asilimia 15 pekee ya malengo hayo na vipengele vyake ndio viko kwenye msitari unaotakiwa.vipengele vya malengo hayo ni 169, lakini Katibu Mkuu ameonya kwamba ni malengo mengi yako nje ya msitari.

Azimio la kisiasa la SDGs

Hivyo amesisitiza kuwa azimio la kisiasa ndio dawa mujarabu wa kusongesha mbele utimizaji na ufikiaji wa malengo hayo ikiwa imesalia chini ya miaka 7 kufika ukomo wake mwaka 2030.

Azimio hilo linajumuisha “ahadi ya kufadhli kwa nchi zinazoendelea ili kusongesha malengo hayo  na msaada mkubwa wa kuunga mkono mapendekezo yake kwa ajili ya SDGs angalu dola bilioni 500 kila mwaka , na pia mkakati wa upunguzaji wa madeni.

Azimio hilo pia linatoa wito wa kubadili mtindo wa biashara wa benki za maendeleo za kimataifa ili kutoa fedha za kibinafsi kwa viwango vya riba nafuu zaidi kwa nchi zinazoendelea, na kuunga mkono mageuzi ya usanifu wa fedha wa kimataifa ambao ameuita umepitwa na wakati, haufanyi kazi vizuri na sio wa haki.

Ufunguzi wa wikiendi ya hatua kwa ajili ya SDGs. Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres akionekana kwenye skrini wakati akitoa hotuba yake
UN Photo/Cia Pak
Ufunguzi wa wikiendi ya hatua kwa ajili ya SDGs. Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres akionekana kwenye skrini wakati akitoa hotuba yake

Mambo sita muhimu ya kuzingatia

Katibu Mkuu huyo wa Umoja wa Mataifa ametaja mambo siku ya muhimu ya kuyatilia maanani kuendeleza mchakato wa utimizaji wa SDGs ambayo ni Mosi ni lazima tuchukue hatua dhidi ya njaa, "Ni shtaka la kila mmoja wetu kwamba mamilioni ya watu wanakufa njaa katika zama hizi na kwenye dunia iliyosheheni kila rasilimali.

Pili kuhamia kwenye nishati jadidifu kunakwenda polepole mno tunaweka mkataba mpya kuhusu nishati.

Tatu faida na fursa za kidijitali hazizambazwi kwa usawa, 

Nne watoto na vijana wenginji wahanga wa elimu duni au kutokuwa na elimu kabisa.

Tano watu wanahitaji kazi zenye staha na ulinzi wa hifadhi ya jamii 

Na sita , Katibu Mkuu amesisitiza kwamba vita dhidi ya asili lazima vikome. na mgogoro wa pande tatu wa sayari Dunia unaojulikana kama mabadiliko ya tabianchi, uchafuzi wa mazingira na upoteve wa bioanuwai.

Mkutano wa SDGs 2023
United Nations
Mkutano wa SDGs 2023

Agano la kujitolea

Rais wa Baraza la Kiuchumi na Kijamii la Umoja wa Mataifa (ECOSOC), Paula Narváez, amesema ametiwa moyo na kupitishwa kwa azimio hilo la kisiasa, na kulitaja kuwa ushuhuda wa dhamira isiyoyumba ya viongozi katika kutekeleza malengo ya SDGs.

ECOSOC ndio msingi wa kazi ya mfumo wa Umoja wa Mataifa kuhusu nguzo zote tatu za maendeleo endelevu  yaani kiuchumi, kijamii na kimazingira na inatoa jukwaa la ufuatiliaji na mapitio ya malengo hayo.

Mkutano huu wa siku mbili wa SDG ni kitovu cha wiki ya ngazi ya juu ya Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, ambao ni mkutano wa kila mwaka wa wakuu wa nchi na serikali.

Kutumia fursa hii

Ameongeza kuwa Mjadala wa ngazi ya juu wa Ufadhili wa Maendeleo utashughulikia hitaji la usanifu wa kimataifa wa kifedha ambao unaweza kujibu mahitaji ya sasa na changamoto zinazoibuka.

Wakati huo huo, Mkutano wa wakuu w anchi kuhusu hatua dhidi ya mabadiliko ya tabianchi unatoa fursa ya maendeleo madhubuti juu ya hatua dhidi ya mabadiliko ya tabianchi na kuongeza kiwango cha juhudi zaidi za wakati na zilizoratibiwa.

"Wiki hii inapaswa kutumika kama hatua ya mageuzi kuokoa SDGs," amesema. "Hatupaswi kuruhusu wakati huu kuteleza."