Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kuvuka baharí ya mediterania imekuwa kama tiketi ya kifo:UNHCR

Waokoaji wa kikosi cha wanamaji cha Italia wakiokoa wahamiaji kwenye bahari ya Mediteranea
Italian Coastguard/Massimo Sestini
Waokoaji wa kikosi cha wanamaji cha Italia wakiokoa wahamiaji kwenye bahari ya Mediteranea

Kuvuka baharí ya mediterania imekuwa kama tiketi ya kifo:UNHCR

Wahamiaji na Wakimbizi

Ikiwa ni miaka mitatu tangu picha za kutisha  za mwili wa mtoto mdogo, Alan Kurdi, akiwa katika ufukwe wa bahari nchini Uturuki  zisambae, ripoti mpya ya shirika la Umoja wa Mataifa la kuwahudumia  wakimbizi, UNHCR  inaonyesha kuwa wakati huu kuvuka baharí ya Mediterania  imekua hatari zaidi inayosababisha vifo kuliko wakati mwingine wowote.

 Ripoti mpya ya UNHCR, iliyopewa jina  “safariza kukatisha tamaa” inaonyesha kuwa  watu zaidi ya 1,600 wamefariki dunia  au kutoweka wakijaribu kwenda Ulaya mwaka huu kupitia baharí hiyo. Ikiongeza kuwa ingawa idadi ya watu wanaosafiri kuingia Ulaya imepungua lakini idadi ya vifo imepanda sana.

 Mediterania ya kati, ripoti inaonyesha mtu mmoja kati ya 18 alifariki dunia au kupotea kwa waliofanikiwa kufika  Ulaya kati ya miezi ya Januari na Julai 2018, ikilinganishwa na  kifo cha mtu mmoja  kwa kila watu 42 waliovuka kipindi cha mwaka wa 2017.

Mkurugenzi wa Ofisi ya UNHCR tawi la Ulaya, Pascale Moreau, amesema kuwa , ripoti hii kwa mara nyingine  inadhihirisha kuwa Mediterania ni  moja wa vivuko hatari zaidi duniani.Ameongeza kuwa kutokana na idadi ya wanaowasili kuingia Ulaya  kupungua, hii sio tena mtihani wa endapo Ulaya itaweza kumudu idadi ya wahamiaji  bali ni endapo Ulaya ina utu wa kuokoa maisha.

Miezi michache iliyopita , UNHCR pamoja na shirika la Umoja wa Mataifa la Uhamiaji IOM,wametoa wito wa kuwepo kwa  mtazamo wa kikanda wa uokozi na kuwapeleka ufukweni watu ambao wako katika shida kwenye baharí ya Mediterania.

Pia UNHCR imeliomba bara Ulaya  kuimarisha mpango wa njia salama na fursa kwa wakimbizi na waomba hifadhi , kuondoa vikwazo dhidi ya watu hao kuunganishwa tena na familia zao na pia kusaidia kupatikana kwa njia mbadala ya ile hatarishi.