Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ubabe wa wajumbe Barazani kuendelea kutesa wasyria

Ubabe wa wajumbe Barazani kuendelea kutesa wasyria

Pakua

Vuta ni kuvute baina ya wajumbe wa Baraza la Usalama kuhusu sakata la madai ya matumizi ya silaha za kemikali huko Douma nchini Syria, imeendelea hii leo baada ya maazimio mawili tofauti yaliyowasilishwa mbele yao mchana wa leo Jumanne kugonga mwamba.

Azimio moja liliwasilishwa na Marekani likilenga kuanzisha jopo huru la Umoja wa Mataifa la kuchunguza matumizi ya silaha za kemikali huko Syria, ilhali azimio lingine liliwasilishwa na Urusi likilenga kuondoa ombwe la uchunguzi lililoibuka baada ya jopo la awali la uchunguzi huko Syria kutoongezewa muda.

Kila upande, yaani Urusi na Marekani, ulitumia kura yake turufu na hivyo kusababisha maazimio yote mawili  yagonge mwamba na kuwaacha wananchi wa Syria katika sintofahamu zaidi.

Mbele ya Baraza la Usalama hii leo mchana, Rais wa chombo hicho kwa mwezi huu wa Aprili Balozi Gustavo Meza-Cuadra kutoka Peru aliwasilisha rasimu ya kwanza ya azimio mezani, azimio lililowasilishwa na Marekani pamoja na wadau wake ikiwemo Canada, Uingereza na Ufaransa.

(Sauti ya Balozi Gustavo Meza-Cuadra)

“Matokeo ni kama ifuatavyo, 12 zimeunga mkono, 2 zimepinga na 1 hakuonyesha upande wowote. Azimio halijapita kwa sababu mjumbe mmoja wa kudumu amepinga.”

Mjumbe aliyepinga azimio hilo ni Urusi ambayo nayo wakati ukawadia muda kwa Rais wa Baraza kuwasilisha rasimu ya azimio lililopendekezwa na Urusi.

(Sauti ya Balozi Gustavo Meza-Cuadra)

“Matokeo ya kura ni kama ifuatavyo, kura 6 zimeunga mkono, 7 zimepinga na 2 hazikuonyesha upande wowote. Rasimu ya azimio haikupita kwa kushindwa kupata idadi ya kura zinazohitajika.”

Ili azimio hilo lipite lilihitaji angalau nusu ya idadi ya kura zilizopigwa ambapo zilizounga mkono ni 6 tu ilhali 7 zimepinga.

Ingawa maazimio hayo yalishasambazwa kwa wajumbe kwa ajili ya kupitia siku za awali, kasi zaidi imeongezeka siku za hivi karibuni baada ya shambulio linalodaiwa kuwa la silaha za kemikali dhidi ya raia tarehe 7 mwezi huu huko Douma, eneo la Ghouta Mashariki nchini Syria.

Audio Duration
2'16"
Photo Credit
OCHA/Ghalia Seifo