Guterres atoa wito wa mageuzi katika ufadhili wa Nchi za Visiwa Vidogo Zinazoendelea
![Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guteres akihutubia wakati wa kufungwa kwa mkutano wa Jukwaa la kimataifa la biashara la nchi zinazoendelea za visiwa vidogo, SIDS huko Antigua na Barbuda Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guteres akihutubia wakati wa kufungwa kwa mkutano wa Jukwaa la kimataifa la biashara la nchi zinazoendelea za visiwa vidogo, SIDS huko Antigua na Barbuda](https://global.unitednations.entermediadb.net/assets/mediadb/services/module/asset/downloads/preset/Libraries/Production%20Library/26-05-2024_Guterres_SIDS_Global%20Business%20Network%20Forum.jpeg/image1024x768.jpg)
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guteres akihutubia wakati wa kufungwa kwa mkutano wa Jukwaa la kimataifa la biashara la nchi zinazoendelea za visiwa vidogo, SIDS huko Antigua na Barbuda
Guterres atoa wito wa mageuzi katika ufadhili wa Nchi za Visiwa Vidogo Zinazoendelea
Ukuaji wa Kiuchumi
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ; António Guterres ameangazia uwezekano wa nchi za Visiwa Vidogo zinazoendelea kukabiliwa na majanga ya tabianchi na kifedha na hivyo akatoa wito wa msamaha wa madeni, mabadiliko ya taratibu za utoaji mikopo na kujumuishwa katika taasisi za fedha za kimataifa ili kusaidia nchi hizi zilizoathirika kwa kiasi kikubwa.
Katika ufunguzi wa mkutano wa ngazi ya juu kuhusu uhamasishaji wa rasilimali kwa Nchi za Visiwa Vidogo Zinazoendelea, SIDS, huko Antigua na Barbuda, Guterres ametoa wito wa kufanyiwa marekebisho mfumo wa fedha wa kimataifa ili kusaidia mataifa haya yaliyo hatarini.
Kikao hicho ni sehemu ya Mkutano wa Nne wa Kimataifa wa Nchi za Visiwa Vidogo Zinazoendelea, SIDS4, uliofanyika katika nchi ambayo ilikumbwa na vimbunga Irma na Maria mwaka 2017.
Dola bilioni 100 za Marekani
Akisisitiza kwamba SIDS nyingi hazina rasilimali za kutosha, Guterres ameangazia athari za janga la Covid-19, uvamizi wa Urusi nchini Ukraine na mabadiliko ya tabianchi, ambayo kwa pamoja yamechangia janga la kifedha na kibinadamu.
Guterres amedokeza kuwa, kati ya mwaka 2010 na 2019, SIDS zilipata hasara ya karibu dola za Marekani bilioni 100 kutokana na majanga ya asili, akibainisha kuwa mataifa hayo yanakabiliwa na changamoto kubwa zaidi katika kufikia Malengo ya Maendeleo Endelevu, SDGs.
Amekosoa mfumo wa fedha wa kimataifa kwa kuziacha nchi hizo zikiwa na mifuko tupu, na kuzifanya zichukue viwango vya juu vya madeni na kufanya rasilimali muhimu ambazo zingeelekea kwa sekta muhimu kama vile afya na elimu kutumika katika ulipaji madeni.
Katibu Mkuu amepongeza mipango inayoongozwa na takwimu kama vile Waziri Mkuu wa Antigua na Barbuda, Gaston Browne, na Waziri Mkuu wa Barbados, Mia Amor Mottley, ambayo inalenga kubadilisha utaratibu wa ukopaji na kuhakikisha ufadhili unaojumuisha na ustahimilivu kwa nchi za visiwa.
Hata hivyo, amesisitiza kuwa pamoja na jitihada za ndani, SIDS bado inakabiliwa na upinzani kutoka kwa taasisi za fedha za kimataifa.
Mpango wa utekelezaji
Guterres amependekeza hatua zichukuliwe katika nyanja tatu: msamaha wa madeni, mabadiliko ya mbinu za ukopeshaji, na ushirikishwaji zaidi katika taasisi za fedha za kimataifa.
Aidha ametoa mwito wa msamaha wa madeni, utekelezaji wa vifungu vinavyohimili tabianchi katika mikopo, na mageuzi ya usanifu wa fedha wa kimataifa ili kuakisi hali halisi ya kiuchumi ya sasa na “kutoa wavu madhubuti wa usalama kwa nchi zinazoendelea.”
Guterres amemalizia kwa kutoa wito kwa jumuiya ya kimataifa kutumia fursa ya Mkutano wa “Siku zijazo” utakaofanyika mwezi Septemba jijini New York, Marekani ili kukuza mfumo endelevu zaidi wa kifedha na shirikishi, akisisitiza kwamba ni wakati wa kuunda mustakabali wa kifedha duniani ambao hauachi nyuma taifa la visiwa.