Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

COVID-19 imekuwa kigingi cha kupambana na usafirishaji haramu wa binadamu: UNODC Ripoti

"Walk For Freedom" ni siku ya uhamasishaji duniani na upiganaji wa hatua za ndani katika mapambano dhidi ya biashara haramu ya binadamu.
© Unsplash/Hermes Rivera
"Walk For Freedom" ni siku ya uhamasishaji duniani na upiganaji wa hatua za ndani katika mapambano dhidi ya biashara haramu ya binadamu.

COVID-19 imekuwa kigingi cha kupambana na usafirishaji haramu wa binadamu: UNODC Ripoti

Sheria na Kuzuia Uhalifu

Ripoti mpya iliyotolewa leo na ofisi ya Umoja wa Mataifa ya madawa na uhalifu UNDOC kuhusu usafirishaji haramu wa binadamu inaelezea hofu kwamba rasilimali za kuwaokoa waathirika wa usafirishaji haramu zimeelekezwa kwenye janga la COVID-19.  

Takwimu za UNODC zinaonyesha kwamba waathirika walioweza kutoroka wamefanya hivyo bila msaada wowote na hofu ni kwamba janga wa COVID-19 limezilazimisha serikali kuelekeza rasilimali za shughuli za polisi kukabiliana na uhalifu huo ikiwemo mitandao ya wasafirishaji haramu na kuwasaka waathirika kwenye janga la COVID-19.  

Ripoti hiyo ya kimataifa inayotolewa kila mwaka imekusanya takwimu kutoka nchi 141na inatoa mtazamo wa mwenendo wa usafirishaji haramu kwa visa vilivyobainika kati ya mwaka 2017 na 2021. 

Matokeo ya utafiti wa ripoti hiyo 

Kwa mujibu wa UNODC matokeo ya utafiti wa ripoti hiyo yanajumuisha tathimini ya kesi 800 zilizo mahakamani na mapendekezo ya kina kwa watunga sera ili kusaidia kuweka mikakati Madhubuti ya hatua kwani janga la COVID-19 ;inaendelea kuweka mazingira mabaya na kudhoofisha uwezo wa kuokoa waathirika na kuwafikisha wahalifu kwenye mkono wa sheria. 

Pia ripoti imebaini kwamba idadi ya waathgirika wa usafirishaji haramu kote duniani ilipungua kwa asilimia 11% na idadi ya hukumu zilizotolewa kutokana na makosa ya usafirishaji haramu wa binadamu pia zilipungua kwa asilimia 27 mwaka 2020, huku ripoti ikionya kwamba masharti wakati wa janga la COVID-19 huenda yaliisukumua baadhi ya mifumo ya usafirishaji haramu wa binadamu kuingia katika maeneo yaliyojificha zaidi. 

Watoto na wanawake bado wako katika hatari kubwa ya usafirishaji haramu barani Asia na Mashariki ya Kati.
© UNICEF/Shehzad Noorani
Watoto na wanawake bado wako katika hatari kubwa ya usafirishaji haramu barani Asia na Mashariki ya Kati.

Hali halisi katika kanda mbalimbali 

Ripoti inasema kupungua kwa kiasi kikubwa kwa hukumu za makosa ya usafirishaji haramu wa binadamu kumeripotiwa Asia Kusnini kwa asilimia 56%, Amerika ya Kati na Caribbea asilimia 54 na Amerika Kusini asilimia 46%. 

Ripoti imesisitiza kwamba vita ya Ukraine inaongeza hatari ya usafirishaji haramu wa binadamu kwa wakimbizi wa ndani ambapo waathirika wengi wa maeneo ya vita wanasafirishwa kiharamu Kwenda nchi za Afrika na Mashariki ya Kati. 

Pia ripoti imesema kuna kiwango kikubwa cha ukwepaji sheria wa makosa ya usafirishaji haramu katika nchi za Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara na Kusini mwa Asia. 

Ripoti imeongeza kuwa katika nchi za kanda hizo kuna wahalifu wachache sana wa usafirishaji haramu wa binadamu wanaohukumiwa na wanabaini waathirika wachache sana wa uhalifu huo kuliko sehemu nyingine duniani.