Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Guterres awaambia waukraine 'dunia inawaona' huku akiahidi msaada zaidi

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres akizungumza na waandishi wa habari pamoja na Rais Volodymyr Zelenskyy wa Ukraine
UN /Eskinder Debebe
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres akizungumza na waandishi wa habari pamoja na Rais Volodymyr Zelenskyy wa Ukraine

Guterres awaambia waukraine 'dunia inawaona' huku akiahidi msaada zaidi

Amani na Usalama

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ameielezea Ukraine kama "kitovu cha maumivu na zahma isiyovumilika", alipozungumza na wanahabari leo mjini Kyiv akiwa pamoja na mwenyeji wake rais Volodymyr Zelenskyy wa Ukraine na kuahidi kuongeza msaada kwa watu wa taifa hilo huku kukiwa na mateso makubwa , na mamilioni ya watu wamekimbia makazi yao kutokana na uvamizi wa Urusi. 

Bwana Guterres amesema mbele ya waandishi Habari hao wanaotoka kila pembe ya dunia kwamba "niko hapa kuangazia njia ambazo Umoja wa Mataifa unaweza kuzitumia kusaidia watu wa Ukraine, kuokoa maisha, kupunguza mateso na kusaidia kutafuta njia ya amani.” 

Muda mfupi baada ya mkutano na waandishi wa habari, mashambulio mawili ya makombora yaliripotiwa kutikisa mji mkuu Kyiv ikiwa ni ukumbusho kwamba vita bado iko mbali sana kumalizika licha ya kujiondoa kwa Urusi kutoka vitongoji vya jirani. 

Mtu mmoja ameripotiwa kuuawa, na wengine kadhaa kujeruhiwa na wengine wakielezwa kufunikwa chini ya kifusi wakati majengo mawili ya ghorofa yalipowaka moto  

Katibu Mkuu wa UN António Guterres akizungumza na wanahabari mjini Kyiv nchini Ukraine
UN /Eskinder Debebe
Katibu Mkuu wa UN António Guterres akizungumza na wanahabari mjini Kyiv nchini Ukraine

Ukraine, dunia haijafumba macho 

Katibu Mkuu ameongeza kuwa "nataka watu wa Ukraine wajue kwamba ulimwengu unawaona, unakusikia, na unastaajabishwa na mnepo mlionao. Pia najua maneno tu ya mshikamano hayatoshi. Niko hapa ili kuangazia mahitaji ya msingi na kuongeza juhudi za operesheni zetu.” 

Akaenda mbali zaidi na kusisitiza kwamba "vita hii  lazima iishe, na amani lazima irejeshwe, kwa mujibu wa katiba ya Umoja wa Mataifa na sheria za kimataifa. Viongozi wengi wamefanya juhudi nyingi nzuri kusitisha mapigano, ingawa juhudi hizi, hadi sasa, hazijazaa matunda. Niko hapa kukuambia, Mheshimiwa Rais, na watu wa Ukraine kwamba, hatutokata tamaa." 

 

Tweet URL

Mgogoro ndani ya mgogoro Mariupol 

Bwana Guterres amesema makumi ya maelfu ya raia na wapiganaji wanaoaminika kuachwa katika mji wa pwani uliozingirwa na kuharibiwa wa Mariupol, wamekuwa na uhitaji mkubwa wa upenyo wa kibinadamu ili kuepuka hofu na shaka dhidi ya uvamizi wa mwisho wa wa Urusi katika kiwanda cha chuma cha Azovstal. 

"Mariupol ni mgogoro ndani ya mgogoro. Maelfu ya raia wanahitaji msaada wa kuokoa maisha. Wengi ni wazee, wanahitaji huduma ya matibabu au wana wameshindwa kuondoka. Wanahitaji njia ya kutoroka kutoka kwenye janga hili.” 

Amekumbusha kuwa katika mkutano wake na Rais Vladimir Putin mjini Moscow siku ya Jumanne, kumekuwa na makubaliano kikanuni ya kuhusisha Umoja wa Mataifa na chama cha msalaba mwekundu, ili kusaidia uhamisho wa raia. 

"Leo, Rais Zelenskyy na mimi tulipata fursa ya kushughulikia suala hili. Tunapozungumza, kuna majadiliano makubwa ya kusonga mbele juu ya pendekezo hili ili liwe litimizwe." 

Katibu Mkuu wa UN António Guterres akitembelea mji  wa Irpin nchini Ukraine
UN /Eskinder Debebe
Katibu Mkuu wa UN António Guterres akitembelea mji wa Irpin nchini Ukraine

Msaada kwa mamilioni 

Katibu Mkuu amesema msaada wa kibinadamu wa kuokoa maisha umewafikia watu milioni 3.4 ndani ya Ukraine, akiongeza kuwa Umoja wa Mataifa unalenga kuongeza zaidi ya mara mbili ya idadi hiyo hadi watu milioni 8.7 ifikapo mwisho wa mwezi Agosti. 

Bwana. Guterres amesema msaada wa pesa taslimu unaongezwa, na Umoja wa Mataifa unagawa dola milioni 100 kwa mwezi, zikilenga kufikia watu milioni 1.3 ifikapo mwisho wa mwezi Mei, na kuwagharamia watu milioni mbili ifikapo mwezi Agosti. 

Leah Mushi/UN News Kiswahili
Nakumbuka familia yangu!!!

"Hii sio operesheni ya kawaida ya kibinadamu ya Umoja wa Mataifa katika nchi inayoendelea, yenye matatizo mengi ya utawala na changamoto nyingine nyingi. Ukraine ni nchi yenye serikali na mfumo unaoungwa mkono  na raia wake, na hivyo jukumu la Umoja wa Mataifa si kuchukua nafasi ya mfumo huo, ni kuunga mkono Serikali kusaidia watu wa Ukraine.” 

Msaada wa chakula umewafikia watu milioni 2.3, amesema Katibu Mkuu, lengo likiwa ni kusaidia watu milioni nne ifikapo mwezi Mei na milioni sita ifikapo mwezi Juni. 

Ameongeza kuwa Umoja wa Mataifa utaongeza uwezo wa kukidhi mahitaji ya watu milioni 7.7 ambao wamehamishwa ndani ya Ukraine, wakati shirika la afya la Umoja wa Mataifa duniani (WHO) likitoa vifaa vya matibabu kwa waliojeruhiwa na huduma za dharura kwa zaidi ya watu milioni saba. 

Mji wa Bucha umesambaratishwa kwa mabomu kutokana na uvamizi wa Urusi nchini Ukraine
UN /Eskinder Debebe
Mji wa Bucha umesambaratishwa kwa mabomu kutokana na uvamizi wa Urusi nchini Ukraine

"Na tunaendeleza kazi ya uwajibikaji na haki kwa kufuatilia na kutoa taarifa juu ya ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu popote inapogunduliwa." 

Bado tuko mbali kuwajibika 

Mwishowe Guterres, amewaambia waandishi wa habari huko Kyiv kwamba, "kwa njia nyingi, bado tuko mwanzo kabisa katika kufikia ulimwengu tunaohitaji kuujenga, ulimwengu wa kuheshimu sheria za kimataifa, mkataba wa Umoja wa Mataifa na nguvu ya mshikamano wa kimataifa, dunia ambayo inalinda raia. , ulimwengu unaoendeleza haki za binadamu, ulimwengu ambamo viongozi wanaishi kwa kuheshimu maadili ambayo wameahidi kuyafuata.”