Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Afrika tusirudi nyuma, teknolojia ya kidijitali tunaiweza na tusikate tamaa- Nanjira

Nanjira Sambuli, mjumbe wa jopo la ngazi ya juu la Umoja wa Mataifa kuhusu ushirikiano wa kidijitali akihojiwa na Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa kando mwa uzinduzi wa ripoti ya kwanza ya jopo hilo. (10 Juni 2019)
UN News/Patrick Newman
Nanjira Sambuli, mjumbe wa jopo la ngazi ya juu la Umoja wa Mataifa kuhusu ushirikiano wa kidijitali akihojiwa na Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa kando mwa uzinduzi wa ripoti ya kwanza ya jopo hilo. (10 Juni 2019)

Afrika tusirudi nyuma, teknolojia ya kidijitali tunaiweza na tusikate tamaa- Nanjira

Malengo ya Maendeleo Endelevu

Afrika imepiga hatua japo kiasi katika  zama za kidijitali hasa masuala ya teknolojia ya mitandao ingawa safari bado ni ndefu.

Kauli hiyo imetolewa na Nanjira Sambuli mjumbe wa jopo la Umoja wa Mataifa la kuhakikisha hakuna anayesalia nyumba katika zama za kidijitali hasa kwa nia ya kusongesha mbele ajenda ya 2030 ya maendeleo endelevu au SDG.

Sambuli ambaye pia ni meneja wa masuala ya será katika mfuko wa kimataifa,  world wide web Foundation akizungumza na Flora Nducha kandoni mwa mkutano wa jopo hilo la ngazi ya juu  baada ya kuwasilisha ripoti yao kwenye Baraza Kuu,  amesema katika zama hizi za kidijitali Afrika ingawa inajikongoja lakini inasonga.

Bi. Sambuli amesema, "tunajaribu, tunaweza sema  takribani asilimia  20 hadi  25 hivi Afrika , tunatumia mtandao wa kidijitali au intaneti. Kuna kazi ambayo tunatakiwa kufanya wote, kampuni zinazofanya kazi Afrika na Afrika mashariki na kwingineko, serikali zetu zina kazi za kufanya kuhakikisha kwamba wanawapa ruzuku kampuni na watu  kuwekeza katika mitandao ya kidijitali. Tumeona kwa sababu ya Mpesa hapo  Afrika Mashariki watu wameanza kuona umuhimu na zile faida wameweza kupata kutokana na mitandao ya kidijitali na imeendeleza mahitaji yao."