Ajali ya Chernobyl bado inatuandama: Vanmarcke
Leo ni miaka 37 tangu ajali ya kinu cha nyuklia cha Chernobyl nchini Ukraine iliyoyosababisha maafa na uharibifu mkubwa wa mazingira kutokana na mabaki ya mionzi ya nyuklia inanyoendelea kusambaa hewani hadi hii leo. Assumpta Massoi na maelezo zaidi.
(Taarifa ya Assumpta Massoi)
Tangu wakati huo watafiti wameendelea kuangazia madhara ya kuvuja kwa mionzi ya nyuklia kutoka kwenye kinu hicho.
Profesa Hans Vanmarcke ambaye ni mkuu wa kamati ya Umoja wa Mataifa kuhusu madhara ya mionzi ya nyuklia, UNSCEAR ameiambia Idhaa ya UN kuwa tangu mwaka 1991 hadi 2015, wamepokea visa vya kansa ya koo kutoka kwa watu elfu 20 ambao waliathirika na mionzi ya nyuklia kutoka Chernobyl.
Watu hao ni kutoka Belarus , Ukraine, ukanda wote wa Ulaya mashariki na Urusi ambako mionzi hiyo ilienea.
(Sauti ya Profesa Hans Vanmarcke)
“Kwa mujibu wa tafiti zetu, moja kati ya visa 4 vya waathirika wa kansa ya koo vinasadikiwa kutokana na ajali ya Chernobyl, kiwango ambacho ni sawa na watu 5000. Tunasema hivyo kwasababu sampuli ya madini joto yatokanayo na mionzi ya Chernobyl yanapatikana katika miili ya watu hao kutokana na kwamba wakiwa watoto walikunywa maji, maziwa na chakula kilichokuwa kimeathirika na mionzi hiyo.”
Na kuhusu uwezekano ya kwamba mwanamke aliyepigwa na mionzi hiyo anaweza kumhamishia mtoto, Profesa Vanmarcke amesema..
(Sauti ya Profesa Hans Vanmarcke)
“Magonjwa ya kurithi ni tofauti na kansa ya koo. Kwa mujibu wa tafiti mbalimbali kwa wanyama inawezekana, ila bado hakuna ushahidi wa binadamu kurithi magonjwa yatokanayo na mionzi ya nyuklia. Hatujaweza kuwa na ushahidi hata kutokana na mabomu ya nyuklia ya Hiroshima na Nagasaki.”