Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kuteketea makazi ya Kotobi ni msumari wa moto juu ya kidonda:UNMISS

Wakimbizi wa ndani wa Sudan Kusini.(Picha:UNMISS)

Kuteketea makazi ya Kotobi ni msumari wa moto juu ya kidonda:UNMISS

Nchini Sudan Kusini baadhi ya jamii za waliotawanywa na machafuko wamejikuta hawana pa kulala baada ya makazi yao kusalia majivu yalipoteketezwa na moto. Kwa mujibu wa mpango wa Umoja wa Mataifa nchini humo UNMISS watu hao awali walilazimika kuhama walikokuwa wakiishi kufuatia operesheni za kijeshi na sasa hawana pa kukimbilia. Siraj Kalyango na tarifa kamili

Mjini Kotobi watoto wakicheza nje ya nyumba zilizoteketea kabisa kwa moto bila kutambua ukubwa wa janga lililokubmba familia zao, lakini kwa wazazi wao wamechanganyikiwa hawana makazi na wamepoteza kila kitu, miezi michache iliyopita machafuko yaliyozuka Kotobi Kaskazini Magharibi mwa Juba yaliwalazimisha mamia ya watu kukimbilia msituni na sasa wamerudi baada ya utulivu kurejea lakini zahma nyingine imewakumba. Juan Tebriwa ni miongoni mwa waliopoteza kila kitu kwa moto huo na kulazimika kukimbia tena

(SAUTI YA JUAN TEBRIWA)

 “Nyumba tulizoziacha Kotobi sasa zimeteketea, tulipofika tulipewa mahema , yote yameharibika na jua, sasa tuko msituni tukilala chini ya miembe, watoto wetu wanishi na hofu kubwa, hakuna mtu yeyote hapa wa kutusaidia kujenga upya nyumba zetu, mume wangu amekufa, lakini tunasalia hapa Kotobi.”

Mpango wa UNMISS unaendelea kushika doroa katika maeneo yaliyoathirika sana na mchafuko ikiwemo Kotobi na imeshatoa tarifa kwa washirika wake ili watu hawa wasaidie. Geoffrey Omon ni kiongozi wa kitengo cha UNMISS eneo hilo

(SAUTI YA GEOFFREY OMON)

Tumeliona hilo kwa sababu raia wametawanywa na walishindwa kulinda nyumba zao, moto wa msituni ulizuka na kuteketeza kabisa idadi kubwa ya nyumba katika eneo hili, na endapo raia watataka kurejea kwenye nyumba zao itabidi waanze upya na wanawaomba wahisani kuwapa msaada wa kibinadamu. Hili ni suala ambalo tutalipeleka Yambio na kwa washirika wetu ili wote tuweze kuchangia katika hali hii.”