Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mtaalam wa UM aitaka Myanmar iwaachilie huru wanaharakati bila masharti

Mtaalam wa UM aitaka Myanmar iwaachilie huru wanaharakati bila masharti

Mtaalam maalum wa Umoja wa Mataifa kuhusu hali ya haki za binadamu nchini Myanmar, Tomás Ojea Quintana, amekaribisha kuachiliwa kwa wafungwa 56 wa dhana kufuatia msamaha wa huruma wa rais, huku akielezea hofu yake kuhusu kuendelea kukamatwa kwa wanaharakati wa haki za binadamu na masharti yanayoambatana na kukamatwa kwao.

Mtaalam huyo ameipongeza serikali kwa kuwaachilia watu hao walofungwa kinyume na sheria na serikali ya zamani ya kijeshi, na kuongeza kuwa kuachiliwa kwao siyo tu muhimu kwa waathirika na familia zao, bali ni muhimu pia kwa harakati zinazoendelea sasa za kurejesha demokrasia na maridhiano ya kitaifa.

Hata hivyo, amesema kuwa kuachiliwa huru kwa wafungwa hao wa dhana ni kitu ambacho kinatakiwa kutendeka kwa misingi ya kanuni zilizopo, na kunatakiwa kutekelezwa mara moja na bila masharti yoyote.

Kipengee cha sheria inayohusika na uhalifu nchini Myanmar inaweka masharti kwa kuachiliwa kwa wafungwa, huku rais akipewa uwezo wa kurejesha kifungo kilichosalia akiamua kuwa mfungwa aliyeachiliwa amekiuka masharti ya kuachiliwa.