Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Waasi wa M23 waripotiwa kukiuka azimio la UM: Waonekana Kivu Kaskazini

Waasi wa M23 waripotiwa kukiuka azimio la UM: Waonekana Kivu Kaskazini

Hali ya usalama katika majimbo ya Kivu Kaskazini na Kivu Kusini imeripotiwa kuwa ni ya wasiwasi baada ya waasi wa kikundi cha M23 kuonekana katika viunga vya mji wa Goma, Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC.

Msemaji wa Umoja wa Mataifa Martini Nesirky amewaambia waandishi wa habari mjini New York, Marekani hii leo kuwa kutokana na ripoti hizo kikosi cha kulinda amani cha umoja huo huko DRC, MONUSCO, mwishoni mwa wiki kiliimarisha doria zake za ardhini na angani.

“Ijapokuwa ripoti nyingi hazikuweza kuthibitishwa, lakini MONUSCO iliweza kuthibitisha uwepo wa waasi wa M23 kwenye maeneo kadhaa jimbo la Kivu Kaskazini ikiwemo karibu na Rwhindi, Kibati na Masisi karibu na Moja. Kitendo hicho ni kinyume na azimio la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa namba 2076. MONUSCO inaendelea na doria zake za mara kwa mara mjini Goma na viunga vyake.”