Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wafanyakazi wazee na vijana wana mchango sawa: ILO

Wafanyakazi wazee na vijana wana mchango sawa: ILO

Sera za kuwafanya watu wastaafu mapema hazijasaidia kuongeza nafasi za ajira kwa vijana, limesema shirika la kazi duniani, ILO. Kwa mujibu wa Mkurugenzi wa ILO kuhusu ajira, José Manuel Salazar, mchango wa watu wazee ni mkubwa katika mazingira ya kazi kama ulivyo wa vijana.

ILO imesema kuwa nchi zenye uchumi ulioendelea zinakabiliwa na changamoto mbili zenye kuhusiana, ambazo ni ukosefu wa ajira kwa vijana, na watu kuishi miaka mingi zaidi.

Kwa mujibu wa Bwana Salazar, ingawa kushusha umri wa watu kustaafu ili vijana wapate nafasi za ajira linaonekana kama suluhisho, mtazamo kama huo unaweza kuwa wa kupotosha, kwani vijana hawawezi kuchukua nafasi za watu wazee kwa urahisi. Amesema mara nyingi mazungumzo yanahusu kuongeza nafasi za ajira kwa vijana, huku watu wazee wakipuuzwa, lakini hali imebadilika na wazee wanahitaji kuzingatiwa kama vile vijana wanavyozingatiwa.