Makubaliano ya biashara ukanda wa pasifiki, TPP kuleta ahueni- UNCTAD
Kamati ya biashara na maendeleo ya Umoja wa Mataifa, UNCTAD imesema mkataba wa biashara baina ya nchi za ukanda wa Pasifiki, TPP utaleta ahueni kubwa ya biashara na kuwezesha kupunguza bei za bidhaa.
Utafiti wa UNCTAD umebainisha kuwa ingawa ni vigumu kutathmini manufaa ya mkataba huo uliotiwa saini mwezi Februari mwaka huu, bado kunaonekana kuwa angalau bei ya bidhaa itapungua.
Mathalani imesema bei ya nyanya ya chupa inayoagizwa kutoka Chile na kuuzwa kwenye soko la Amerika ya kaskazini itakuwa nafuu kwa asilimia 12 ikilinganishwa na sasa.
Mkataba huo ulitiwa saini na Australia, Brunei, Canada, Chile, Japan, Malaysia, Mexico, New Zealand, Peru, Singapore, Vietnam na Marekani lakini hadi sasa hakuna nchi ambayo imeridhia ambapo UNCTAD inasema uamuzi wa kisiasa ndio utaamua hatma yake TPP.