Vyama vya ushirika vyawezesha wakulima kufikia masoko Ulaya
Mustakbala wa kazi unaotegemea ajira na uzalishaji endelevu.
Vyama vya ushirika ni muarobaini wa kuwa na uzalishaji na ulaji endelevu.
Huo ni ujumbe wa mkuu wa kitengo wa masuala ya vyama vya ushirika kwenye shirika la kazi duniani, ILO Simel Esim katika siku ya vyama vya ushirika duniani hii leo.
Ametolea mfano wa Sri Lanka akisema baada ya vita vya wenyewe kwa wenyewe vyama vya ushirika vimewezesha mnepo wa jamii na kureje katika hali ya kawaida.
Amesema tathmini ya ILO ilibaini kuwa vyama vya ushirika ndio vilikuwa na miundo thabiti kaskazini mwa nchi hiyi Sri Lanka , kabla, wakati na baada ya mgogoro. Ni kupitia ILO sasa tangu mwaka wa 2010, mradi wa shirika hilo umekuwa ukisaidia vyama vya ushirika vya kilimo na uvuvi kwa kuwapatia uthibitisho bora wa bidhaa zao na pia kuwasaidia kuwapatia soko.
Esim ametaja pia Kenya ambako vyama vya ushirika vimesaidia wakulima na wazalishaji kahawa nchini humo kupenyeza kahawa yao kwenye soko la Denmark.
Halikadhalika ushirika wa vijana nchini Togo umewasaidia mananasi yao kuuzwa rejareja nchini Italia.
Mkuu huyo wa kitengo cha ushirika cha ILO amesema ni kwa kuzingatia manufaa ya ushirika ndio maana ILO inaendelea kupigia chepuo miradi ya baadaye inayolenga vyama vya ushirika kwa lengo la kuhimiza pia miradi isiyoharibu mazingira na ulaji na uzalishaji endelevu.