Maldives zingatia katiba ya nchi- Guterres
Amkani si shwari tena huko Maldives na Umoja wa Mataifa umepaza sauti ili serikali ihakikishe usalama wa raia pamoja na wafanyakazi wa mahakama.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ana wasiwasi mkubwa kuhusu hali ya kisiasa inavyoendelea kwenye visiwa vya Maldives.
Wasiwasi huo unafuatia ripoti za vyombo vya habari kuwa Rais wa Maldives Abdullah Yameen ametangaza hali ya hatari huku Jaji Mkuu akiwa na ameswekwa korokoroni na vikosi vya usalama vimezingira eneo la Mahakama Kuu nchini humo.
Ghasia zimeibuka baada ya waandamanaji kutaka serikali iwaachie huru wafungwa wa kisiasa jambo ambalo linapingwa na serikali ya sasa.
Kupitia msemaji wake, Katibu Mkuu Guterres ameitaka serikali ya Maldives izingatie katiba na utawala wa sheria na wakati huo huo iondoe amri yake ya hali ya hatari.
Badala yake ameitaka ichukue hatua zote kuhakikisha usalama wa raia wakiwemo wafanyakazi wa mahakama.