UN na AU zafuatilia hali ya kisiasa Guinea- Bissau
Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres na mwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika Moussa Faki Mahamat wameendelea kuwa na wasiwasi juu ya mgogoro wa kisiasa wa muda mrefu nchini Guinea-Bissau licha ya jitihada za jamii ya kimataifa za kujaribu mbinu za upatanisho baina ya vyama vya kisasa nchini humo.
Bwana Guterres na Bwana Moussa Faki wamelaani kitendo cha serikali ya nchi hiyo kuzuia chama pinzani cha kisiasa cha PAIGC kisifane kongamano kuu la mwaka la kisiasa, kitu ambacho wamesema ni ukiukwaji wa haki ya kijieleza na pia ukiukwaji wa haki ya vyama vya kisiasia kufanya shughuli zao bila kuingiliwa na vyombo vya ulinzi.
Kupitia taarifa yao ya pamoja viongozi hao wamesema wanaunga mkono kikamilifu uamuzi wa hivi karibuni wa wakuu wa nchi na serikali za Jumuiya ya uchumi za nchi za magharibi mwa Afrika (ECOWAS) katika mkutano wa Umoja wa Afrika huko Addis Ababa, Ethiopia, tarehe 27 Januari, ya kuitaka Guinea Bissau irejee azimio la tarehe 30 januari la Conakry.
Azimio hilo linataka uteuzi wa pamoja wa waziri mkuu mwenye msimamo wa kati na kutaka wadau wa kisiasa kutekeleza mkataba huo kwa uaminifu na kwa haraka, pamoja na mwongozo wa ECOWAS ambao wote wamejiunga.
Wakuu hao wamesema wataendelea kufuatilia kwa ukaribu maendeleo nchini Guinea Bissau na kuwezesha ECOWAS katika jitihada zake za kuhakikisha uamuzi wa haraka wa mgogoro wa muda mrefu nchini humo.
Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa Guinea Bissau imekuwa katika mzozo wa kisiasa tangu mwaka 1974.