Mradi wa shanga huko Kakuma wainua wenyeji wanaohijfadhi wakimbizi
Wakimbizi na jamii zinazowahifadhi nchini Kenya, wamepata mbinu ya kujipatia kipato huko Kolobeyei, kambi ya Kakuma kufuatia ufadhili wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR nchini humo na wadau wengine ikiwemo serikali ya Marekani. Patrick Newman na maelezo zaidi.
Mradi huo wa UNHCR na wadau unawapatia wakimbizi na wanajamii wanaowahifadhi vifaa kwa ajili ya kushona shanga ambazo zinauzwa kwenye kituo cha wageni kambini.
Regina Nanok, miongoni mwa wenyeji wanaopatia hifadhi wakimbizi, ni mmoja wa wanufaika wa mradi huu anasema, "ninashona ushanga wa wanawake. Ninakopata ushanga, ni UNHCR wanatufadhili wanatuletea vifaa na tunatengeneza, wageni wakija tunawauzia. Inatuchukua kama siku mbili kutengeneza. Kwa mkufu tunauza 800 fedha ya Kenya, na kwa hereni tunauza 200."
Bi Nanok hakuficha furaha yake kuhusu faida za mradi, "kwasababu hii kazi inanisaidia mahitaji yangu ninawalisha watoto na inasaidia kazi zangu nyingine za pembeni, ningependa kuishukuru UNHCR kutuwekea kituo hiki na pia niishukuru serikali ya Marekani kwa kuwafadhili hawa ndiyo wakatuwekea kituo hiki cha kuwasaidia wakimbizi."