Kongamano lafanyika Dodoma kujadili sekta ya kilimo, uvuvi na mifugo Tanzania
Mabadiliko ya tabianchi ni moja ya majanga yanayokumba dunia hivi sasa na kuathiri sekta mbalimbali ikiwemo kilimo, ufugaji na uvuvi. Nchini Tanzania kwa kutambua athari hizo hasi, kumefanyika kongamano la nane la mwaka 2022 la sera kwa wadau wa sekta hizo, kongamano lilofanyika katika mji mkuu wa taifa hilo, Dodoma.
Washiriki takribani 600 wametoka mikoa na pande mbalimbali ikiwemo shirika la Umoja wa Mataifa la chakula na kilimo, FAO Tanzania, serikali na sekta binafsi.
Mathalani wadau kutoka sekta binafsi wametoa wito kwa serikali kuwashirikisha katika mapitio ya sera mpya ya kilimo, mifugo na uvuvi ili waweze kutoa mawazo yao yatakayosaidia kukabiliana na changamoto zinazokabili sekta hizo zinazotokana na mabadiliko ya tabianchi. Lakini kwa kina tuungane na Devotha Songorwa wa Redio washirika KidsTime FM nchini Tanzania ambaye alikuwa shuhuda wetu kwenye kongamano hilo.