Zamani tulipeleka watoto kliniki muda tuliopenda lakini mafunzo ya TAMWA yametufungua- Mwanzo Mgumu
Afya ya mama na mtoto ni jambo muhimu katika kuhakikisha kuwa jamii inakuwa na nguvu kazi bora. Afya hii huanzia tangu hata kabla ya ujauzito hadi ujauzito wenyewe, kujifungua na hata baada ya kujifungua. Umoja wa Mataifa unatambua changamoto walizo nazo wanawake hususan maeneo ya mashinani katika kupata huduma bora za afya ya uzazi ikiwemo lishe bora kwa mjamzito na pia kwenda kliniki ili kufahamu maendeleo ya mtoto aliye tumboni. Ni kwa kutambua changamoto hizo wadau wa Umoja wa Mataifa yakiwemo mashirika yasiyo ya kiserikali kama vile chama cha wanahabari wanawake Tanzania, TAMWA tawi la Zanzibar huendesha mafunzo kwa vikundi mashinani. Miongoni mwa vikundi hivyo ni Mwanzo Mgumu kilichoko eneo la Kidoti wilaya ya Kaskazini A, Unguja Zanzibar Tanzania. Assumpta Massoi alitembelea eneo hilo kutaka kufahamu kwa kina mafunzo hayo na yaliwasaidia vipi na hapa mwenyekiti wa kikundi Fatuma Ally Heri anafungua mjadala kwa kujitambulisha na kisha mjadala unaendelea.