Hali itakuwa mbaya zaidi DRC bila misaada ya kibinadamu-Lowcock.
Bila msaada wa kibinadamu maisha ya raia wengi nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) yako mashakani. Onyo hilo limetolewa na Msaidizi wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa anaehusika na masuala ya kuratibu misaada ya kibinadamu , Mark Lowcock wakati akilihutubia baraza la usalama la Umoja wa Mataifa hii leo na kuelezea hali ilivyo DRC.
Katika hotuba yake, amesema kuwa msaada wa kibinadamu unahitajika haraka na laa sivyo hali itakuwa mbaya zaidi. Naye mwanaharakati kutoka mashinani Goma Mashariki mwa DRC, Janine Bandu Bahati akizungumza katika mkutano huo ameelezea hali tete inayowakabili wanawake.
(SAUTI YA BANDU BAHATI)
“Hali ya kiusalama na kibinadamu kwa wanawake nchini DRC inaendelea kudhalilisha, na ni ya vurugu tupu. Watu wengi walioathirika wamejawa na kiwewe, hawana matumaini ya kesho, na sanasana wanawake waishio katika sehemu za mashambani tunakofanyia kazi.”
Awali Bwana Lowcok aliliambia baraza la usalama kuwa mahitaji ya kibinadamu DRC yameongezeka kuliko mwaka jana na watu wanaohitaji msaada kwa sasa ni milioni 13. Huku watoto zaidi ya milioni 4.6 wanakabiliwa na utapiamlo wakiwemo wengine milioni 2.2 wenye ukosefu wa lishe. Ameongeza kuwa magonjwa mbalimbali yanachipuka kama uyoga ambapo kipindupindu kibaya zaidi kutokea kwa miaka 15 kimelipuka hivi karibuni.
Umoja wa Mataifa unalenga kuwasaidia watu milioni 10.5 na kuweza kuishughukilia changamoto hiyo unnahitaji dola bilioni 1.7 kiasi ambacho ni mara nne zaidi ya kile walichohitaji mwaka uliopita.
Mwanaharakati amelielezea baraza la uslama la Umoja wa mataifa kuhusu madhila yanayowakuta wanawake na wasichana mashariki mwa nchi hiyo.