Mfumo waanzishwa kudhibiti uvuvi wa kupindukia wa samaki
Umoja wa Mataifa umeanzisha mfumo wa aina yake wa kubadilishana taarifa za uvuvi kama njia mojawapo ya kudhibiti uvuvi wa kupindukia unaohatarisha uwepo wa samaki duniani.
Kituo cha uwezeshaji biashara cha Umoja wa Mataifa kimesema biashara ya samaki inakadiriwa kuwa na thamani ya dola bilioni 140, lakini biashara hiyo iko hatarini kutokanana uvuvi wa kupindukia na uvuvi haramu.
Katika taarifa yake kituo hicho kimesema hali inakuwa mbaya zaidi kwa kuwa ripoti zozote kuhusu mienendo ya uvuvi zipo kwenye karatasi na kufanya vigumu nchi au taasisi kuweza kuzipata na kufuatilia.
Ni kwa mantiki hiyo wameanzisha mfumo wa kisasa wa kubadilishana taarifa kama vile vyombo vya uvuvi, mienendo yao ya safari, takwimu kuhusu samaki, leseni na takwimu za ukaguzi, mfumo ambao utasaidia kulinda maeneo ambayo tayari samaki wamepungua.