Vijana tusiwe watazamaji bali tuchukue hatua kwa kuanza na tulicho nacho- Emmanuel
Vijana wana dhima kubwa katika kusongesha malengo ya maendeleo endelevu, SDGs yanayofikia ukomo mwaka 2030. Mashirika ya Umoja wa Mataifa kwa kutambua nafasi hiyo ya vijana wanatumia vijana wenyewe ili wawe mabalozi wa mashirika hayo mashinani ili kupigia chepuo yale yaliyomo kwenye SDGs. Mathalani nchini Tanzania shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF lina mabalozi na miongoni mwao ni Emmanuel Cosmas Msoka yeye akijikita kwenye masuala ya usafi wa maji, usafi wa mazingira (WASH) na ubunifu. Na ndiye tunammulika leo katika makala ambapo katika mahojiano naFlora Nducha wa Idhaa hii ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa, Emmanuel ambaye mwezi Septemba mwaka huu alishiriki vikao vya ngazi ya juu vya vijana kuhusu malengo ya maendeleo endelevu, SDGs alielezea mambo kadhaa akianza na kile alichoondoka nacho.