Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan kuhudhuria Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa

Balozi Liberata R. Mulamula, Waziri wa Mambo ya nje na Ushirikiano wa Kimataifa akihojiwa na Leah Mushi wa Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa.
UN News/Anold Kayanda
Balozi Liberata R. Mulamula, Waziri wa Mambo ya nje na Ushirikiano wa Kimataifa akihojiwa na Leah Mushi wa Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa.

Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan kuhudhuria Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa

Masuala ya UM

Kwa mara ya kwanza rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kushiriki katika Baraka kuu la Umoja wa Mataifa linalotarajia kuanza tarehe 21 mpaka 27 Septemba 2022.

Akihojiwa na Leah Mushi wa idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa jijini New York Marekani, Waziri wa Mambo ya nje na Ushirikiano wa Kimataifa Balozi Liberata Mulamula amesema kwas asa wanasubiria maamuzi ya serikali ya Marekani na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa iwapo nchi wanachama watashiriki kwa njia ya mtandao au watasafiri kwenda nchini Marekani.

“Taadhima yetu ni kushiriki, iwe ana kwa ana au mtandao, Muheshimiwa rais ameshasema atashiriki. Na unajua hii ndio mara yake ya kwanza anashiriki kama Rais w anchi atakuja”

Kuhusu vipaumbele vya nchi ya Tanzania katika malengo ya maendeleo endelevu SDGs Balozi Mulamula amesema janga la Corona limerudisha nyuma kasi ya kufikia malengo si kwa Tanzania pekee bali nchi nyingi duniani.

“Kasi imepungua lakini bado tumejipanga kwa mikakati ambayo inagusa malengo yote 17 ya SDGs. Na katika kikao hikio ilipangwa wakuu wa nchi kukaa na kujadili namna walivyotekeleza malengo hayo kujadili kwa pamoja wamefikia wapi na wamekwama wapi. “

Balozi Mulamula ameongeza kuwa “Tayari nchi yetu imeshawasilisha ripoti ya kuonesha jinsi Tanzania ilivyotekeleza. Na katika mazungumzo yangu na rais wa ECOSOC amefurahishwa kwamba sisi ni miongoni mwa nchi chache duniani ambazo tumeweza kutoa taarifa yetu ya utekelezaji wa malengo ya maendeleo endelevu SDGs.”

Nafasi ya mwanamke Tanzania

Akizungumzia kuhusu kumuinua mwanamke, Balozi huyo wa mambo ya nje wa Tanzania amesema pamoja na kuwa na rais mwanamke kalini hawawezi kusema wameshafanya mapinduzi makubwa ila wanachofanya ni kuhakikisha wanatoa fursa kwa wanawake wenye sifa na vijana wengi zaidi katika nafasi za uongozi.

“Kuwa na mwana mama katika nafasi ya urais ni kwamba mapinduzi yanakuja, na utaona katika nafasi mbalimbali za uteuzi amewapa kipaumbele wanawake, wanawake ambao wanaweza.”

Akiwa mwanamke wa pili kushika nafasi ya waziri wa mambo ya nje wa Tanzania, Balozi Mulamula amewatumia ujumbe watanzania na vijana wote akiwasili kuzingatia siri kuu mbili

“Mosi ni elimu, huwezi sema utafanikiwa kwa njia ya mkato, hatakama kuna watu wengi matajiri duniani wamefanikiwa bila kuwa na elimu ni muhimu zaidi kuwa na elimu. Pili ni kufanya kazi kwa bidii, uwe na tabia njema na ufatilie fursa pale zitakapo jitokeza usione aibu.”

Akizungumzia suala la janga la Corona au COVID-19 Balozi Mulamula amesema pamoja na kuwa wanashukuru kupata msaada wa chanjo kutoka kwa wadau mbalimbali ikiwemo serikali ya Marekani lakini wanataka kujengewa uwezo zaidi.

“Kupitia mazungumzo yanu na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres atusaidie tuwezeshwe ili tuwe na viwanda vyetu ili tuweze kutengeneza chanjo zetu wenyewe. Utaona mfano nchi ya India ilivyaothirka na janga la Corona lakini kwakuwa walikuwa wanatengeneza wenyewe chanjo ilikuwa ina uhafadhali kidogo, na sisi tunatamani tufikie huko.”

Hata hivyo ameviomba vyombo vya habari na wadau wengine kuzidi kuwaelimisha wananchi umuhimu wa kupata chanjo kwakuwa bado nchini Tanzania kuna baadhi ya watu wanaamini chanjo zitawaletea madhara. Amesema dhamira ya serikali ni wananchi wao waelewe hakuna njia nyingine bila chanjo, na anaamini kupitia kampeni mbalimbali zinazoendelea watu wataona umuhimu wake na kupata chanjo ya kujikinga na janga la Corona.