Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Habari kwa ufupi: Gaza, Sudan, Mifumo ya chakula

UNICEF inawasaidia watoto waliokimbia makazi yao huko Gaza kutabasamu na kurejesha matumaini kwa kuandaa shughuli za burudani katika makazi. (Maktaba)
Photo: UNICEF/Loulou d'Aki
UNICEF inawasaidia watoto waliokimbia makazi yao huko Gaza kutabasamu na kurejesha matumaini kwa kuandaa shughuli za burudani katika makazi. (Maktaba)

Habari kwa ufupi: Gaza, Sudan, Mifumo ya chakula

Amani na Usalama

Leo Umoja wa Mataifa umeonya kwamba Gaza ni mahali hatari zaidi kuishi kwa watoto. Akizungumza na waandishi wa habari mjini Geneva Uswis msemaji wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF, James Elder amesema  “Siku baada ya siku ukatili wa hali ya juu unadhihirika. Katika saa 48 zilizopita hospitali kubwa Zaidi iliyobaki inafanyakazi imeshambuliwa mara mbili. Hospitali hiyo ya Al Nasser iliyopo Khan Yunis sio tu kwamba inahifadhi idadi kubwa ya Watoto ambao tayari wamejeruhiwa vibaya katika mashambulizi majumbani kwao lakini pia inahifadhi mamia ya wanawake na Watoto wanaosaka usalama.”

Nalo shirika la Umoja wa Mataifa la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina UNRWA limesema zaidi ya asilimia 60 ya mioundombinu Gaza imesambaratishwa kabisa na zaidi ya asilimia 90 ya watu wametawanywa .

Wakimbizi kutoka Darfur wakiwa wamekusanyika kwenye kambini baada ya kuvuka mpaka kutoka Sudan na kuingia Chad. (Maktaba)
© UNHCR/Jutta Seidel
Wakimbizi kutoka Darfur wakiwa wamekusanyika kwenye kambini baada ya kuvuka mpaka kutoka Sudan na kuingia Chad. (Maktaba)

Wimbi kubwa la watu wakimbia mizozo Sudan

Nchini Sudan shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR leo limesema linatiwa wasiwasi kubwa na kiwango cha janga la watu wanaoendelea kulazimika kutawanywa ndani ya Sudan na katika nchi Jirani. Shirika hilo limesema mamia kwa maelfu ya watu wamefurushwa makwao katika mapigano mapya kwenye jimbo la katikati mwa Sudan la Al Jazirah lililoko Kusini Mashariki mwa mji mkuu, Khartoum.

Uzalishaji na utumiaji wa chakula ni chachu ya afya na mazingira
© Unsplash/Anna Pelzer
Uzalishaji na utumiaji wa chakula ni chachu ya afya na mazingira

Mifumo ya Chakula

Na ripoti mpya "Hali ya mifumo ya chakula duniani kote katika kuelekea mwaka  2030", iliyochapishwa leo na mradi wa shirika la chakula na kilimo la Umoja wa Mataifa FAO unaoangia mifumo hiyo kuelekea ukomo wa malengo ya maendeleo endelevu ifikapo mwaka 2030 (FSCI), inatoa tathimini ya kwanza ya ufuatiliaji wa kisayansi ili kuwaongoza watoa maamuzi wanapotaka kufanya mabadiliko ya jumla ya kilimo cha kimataifa na mifumo ya chakula. 

FAO inasema mabadiliko haya yanahitajika haraka ili kupunguza athari za mazingira za mifumo hii ya chakula na za mabadiliko ya tabianchi. Lengo kuu ni kwamba watu wote haswa walio hatarini zaidi wapate fursa sawa ya lishe bora kupitia kilimo endelevu na chenye mnepo na mifumo bora ya chakula.