Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kabila la watwa nchini DRC wasalimisha mishale 3000

Baadhi ya mishale iliyosalimishwa na watu wa kabila la watwa huko DRC. (Picha:MONUSCO)

Kabila la watwa nchini DRC wasalimisha mishale 3000

Wanamgambo wa kabila la watwa huko Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC wamesalimisha mishale 3,000.

Mishale hiyo ilikuwa inatumika kwenye mapigano ya kikabila kati yao ya na jamii wa kabila la wabantu kwenye eneo la Manono lililopo jimbo la Tanganyika.

Msimamizi wa eneo la Manono Pierre Mukamba amesema hatua hiyo ya kusalimisha silaha hizo za kijadi inafuatia mashauriano kati ya ofisi yake na kabila hilo la watwa na tayari silaha hizo zimeteketezwa.

Amesema walifanya mashauriano baada ya kubaini kuwa kabila hilo la watwa walikuwa wamekusanya silaha hizo za jadi tayari kupambamba na wabantu ili kulipiza kisasi cha ndugu zao waliouawa.

Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini DRC, MONUSCO kila mara umekuwa na wasiwasi kutokana na hali ya mapigano ya kikabila huko Manono ambapo umekuwa mstari wa mbele kusaidia mashauriano yanayoweza kuleta amani.

Mathalani MONUSCO huendesha kampeni za kuhamasisha dhidi ya chuki baina ya makabila pamoja na kuendesha doria kulinda usalama.