Hapa na pale
Kwenye taarifa aliotoa KM Ban Ki-moon Ijumanne, kwa waandishi habari, alielezea kuvunjika moyo juu ya kuendelea kwa vitendo visio halali vya Israel, kwenye eneo liliokaliwa kimabavu la Jerusalem Mashariki, ambapo alisema nyumba za WaFalastina zilibomolewa kihorera, na aila kadha zilifukuzwa kutoka majumbani mwao, mastakimu ambayo baadaye walikabidhiwa walowezi wa Kiisraili waliojisakama, kwa nguvu, katika mitaa ya WaFalastina. Vitendo hivi, alionya KM, ni miongoni mwa mambo yenye kupalilia mazingira ya wasiwasi na kudhoofisha zaidi hali ya kuaminiana miongoni mwa makundi yanayohusika na mvutano wa Mashariki ya Kati. Aliisihi Israel kusitisha, halan, vitendo hivi vya uchokozi. Kadhalika, KM alitoa mwito ziada unaoitaka Israel kutekeleza zile ahadi ilizotoa kabla, kuhusu mapendekezo ya Ramani ya Amani juu ya Suala la Mashariki ya Kati, na kusimamisha shughuli zake zote kwenye makazi ya walowezi, ikijumlisha pia vile vitendo vya kutaka kupanua zaidi majengo yaliopo kwenye maeneo yaliokaliwa; na vile vile Israel ilinasihiwa ing\'oe haraka vituo vyote vya mbali vya uangalizi na, hatimaye, iruhusu taasisi za KiFalastina zifunguliwe baada ya kufungwa kwa kitambo, ili zianze kuendesha shughuli zake halali katika eneo la Jerusalem Mashariki.